Habari

Hofu tele wasichana 36 wa shule moja ya Upili wakipata mimba

Na ROSE WANGUI September 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WADAU wa elimu pamoja na viongozi wa utawala katika Kaunti Ndogo ya Webuye Mashariki, Kaunti ya Bungoma, juzi walifanya mkutano wa dharura kufuatia ongezeko kubwa la mimba za mapema katika shule moja ya eneo hilo.

Wanafunzi wasiopungua 36 wa Shule ya Sekondari ya Bakisa wamekuwa wajawazito au wameacha masomo mwaka huu baada ya kupata watoto.

Kwa mujibu wa takwimu zilizowasilishwa na uongozi wa shule hiyo, wanafunzi 10 kwa sasa ni wajawazito na bado wanaendelea na masomo yao huku wakikabiliana na changamoto za ujauzito.

 

Wengine 13 walijifungua majuzi, huku wanafunzi 13 zaidi wakiacha shule kabisa baada ya kupata mimba.

Mkutano huo uliofanyika Ndivisi uliwaleta pamoja maafisa wa usalama, viongozi wa elimu, wazazi, viongozi wa kidini na wanasiasa ili kutafuta suluhu za haraka za kukabili tatizo hilo.

Akizungumza katika mkutano huo, Naibu Kamishna wa Kaunti wa Ndivisi, Emmanuel Kenga, alisema umaskini uliokithiri na uzembe wa baadhi ya wazazi ni miongoni mwa sababu kuu zinazochangia kuongezeka kwa mimba za mapema.

Alisema kuna wanaume wanaowalenga wasichana wadogo kwa kuwapa chakula, zawadi ndogo na fedha ili kushawishi kushiriki ngono.

“Umaskini unachangia sana tatizo hili. Baadhi ya wanaume wanatumia udhaifu wa wasichana wetu kwa kuwavutia kwa pesa na mahitaji ya msingi,” alisema Kenga.

Aidha, alitaja matumizi yasiyodhibitiwa ya simu za mkononi na teknolojia kama sababu nyingine inayowafanya watoto kukumbana na maudhui yasiyofaa katika umri mdogo.

Baadhi ya wazazi waliodhuria mkutano huo walidai kwamba wasichana wengi hushawishiwa na wanaume wanapokuwa njiani kuelekea au wakitoka shuleni. Wengine walilaumu hali ya watoto kulelewa na babu na nyanya huku wazazi wao wakitafuta ajira mijini.

Viongozi wa utawala walifichua kuwa baadhi ya familia hukubali fidia kutoka kwa wanaodaiwa kuwapa mimba watoto wao badala ya kuripoti kesi hizo ili hatua za kisheria zichukuliwe.

Inadaiwa kwamba kesi nyingi hutatuliwa kupitia mikutano ya kijamii au baraza za wazee kwa makubaliano ya kifedha.

Mwalimu Margaret Muindi aliwataka wazazi kukoma kupokea zawadi au fedha kutoka kwa wahusika wa vitendo hivyo kwa kuwa hatua hiyo huathiri juhudi za kupata haki kwa waathiriwa.

Naye Nancy Chibeu, alionyesha masikitiko yake akisema kuwa licha ya wanafunzi 36 kuathiriwa, ni kesi moja pekee ambayo imeripotiwa rasmi.

Alitoa wito kwa wananchi kuwafichua wahusika ili wachukuliwe hatua za kisheria na wasichana walindwe dhidi ya unyanyasaji wa kingono.