• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Agizo la Rais laleta tumaini na shaka kwa wanaspoti

Agizo la Rais laleta tumaini na shaka kwa wanaspoti

Na CHRIS ADUNGO

AGIZO la Rais Uhuru Kenyatta kwamba timu zote za kitaifa zitakazowakilisha Kenya katika mashindano ya kimataifa zifadhiliwe na serikali limeibua hisia mseto miongoni mwa wadau.

Akizungumza mwishoni mwa makala ya nne ya mbio za Beyond Zero Marathon wikendi iliyopita, Rais aliwahakikishia wanamichezo kuwa serikali yake itafadhili vikosi vyote vitakavyowania mataji mbalimbali katika majukwaa ya kimataifa.

“Michezo na sanaa ni sehemu muhimu ya utamaduni wetu. Ni sekta ambayo haiwezi kabisa kuachwa mikononi mwa wahisani pekee,” akatanguliza Rais Kenyatta.

“Mwaka huu 2019, Harambee Stars haitaomba wala kukopa fedha. Itafadhiliwa kikamilifu na serikali. Timu za taifa za raga, voliboli, mpira wa pete na nyinginezo zote zitafadhiliwa kikamilifu na serikali,” akaongeza kiongozi wa nchi na kusisitiza kwamba wanariadha pia watafadhiliwa na hawatakosa sare wala viatu kila watakapokuwa wakipeperusha bendera ya Kenya katika mashindano ya kimataifa.

Agizo hilo la Rais linatolewa wakati ambapo Wizara ya Michezo bado inajizatiti kuhakikisha kwamba mashirikisho yote ya michezo yanazingatia Sheria za Michezo zilizopitishwa na Bunge mnamo 2013.

Ni chini ya sheria hiyo ambapo Hazina ya Michezo ilibuniwa kwa lengo la kuimarisha miundo-mbinu, ujenzi wa miundo-misingi na kuboresha maslahi ya wanamichezo.

Kufufua Shujaa

Kwa mujibu wa Richard Omwela ambaye ni Mwenyekiti wa Shirikisho la Raga (KRU), agizo la Rais litachangia pakubwa katika ufufuo wa kikosi cha Shujaa ambacho kimeshuka pakubwa kimataifa.

Mbali na kuvuta mkia katika duru ya Vancouver Sevens nchini Canada wikendi jana, Shujaa waliteremka hadi nambari 14 baada ya kupoteza mechi tano mfululizo kwa kupepetwa 47-7 na Australia katika robo-fainali ya Challenge Trophy na 22-14 dhidi ya Japan katika nusu-fainali ya kutafuta mshindi wa nambari 13 hadi 16. Awali walizabwa na Fiji (36-12), Samoa (35-12) na Canada (36-21) mechi za makundi.

Kwa pamoja na kocha Paul Murunga, Omwela anaamini kwamba mchango wa serikali utapigisha Shujaa hatua zaidi katika kampeni za duru zijazo za Hong Kong (Aprili 5-7), Singapore (Aprili 13-14), Uingereza (Mei 25-26) na Ufaransa (Juni 1-2).

Kenya imekuwa moja ya timu zinazoshiriki duru zote kwa misimu 16 mfululizo tangu 2002-2003. Ingawa hivyo, imekuwa ikining’inia padogo msimu huu baada ya wachezaji wazoefu kugoma wakilalamikia kupunguziwa mshahara.

Kwa upande wake, Nick Mwendwa ambaye ni Rais wa Shirikisho la Soka (FKF), amesema serikali bado haijajibu ombi lao la kuwasafirisha wanasoka wa Harambee Stars wanaochezea ng’ambo kwa mechi ijayo dhidi ya Ghana.

Ratiba

Stars wameratibiwa kuchuana na Ghana katika mchuano wa mwisho wa Kundi F wa kufuzu kwa fainali za Kombe la Afrika (AFCON) zitakazoandaliwa nchini Misri kati ya Juni 21 na Julai 29.

Ni matumaini ya Katibu wa Shirikisho la Voliboli (KVF), Ben Juma kwamba serikali itawapa Sh55 milioni wanazozihitaji kufanikisha maandalizi ya Malkia Strikers kwa mechi za kimataifa mwaka 2019.

Mbali na Kombe la Dunia nchini Japan mnamo Septemba, Malkia Strikers watashiriki mchujo wa Kombe la Afrika na Olimpiki za Tokyo, Japan mnamo 2020.

Kenya imepangiwa pia kuwania ubingwa wa Voliboli ya Ufukweni kwa Chipukizi wasiozidi umri wa miaka 21 nchini Algeria mnamo Aprili 2019.

Licha ya matumaini hayo ya Juma, Lucas Maranga ambaye ni Mwenyekiti wa Shirikisho la Gofu (KGU) amesema itakuwa vigumu kwa serikali kutekeleza agizo la Rais Kenyatta hasa ikizingatiwa wepesi wa wanasiasa katika kutoa ahadi bila ya kuzitimiza.

You can share this post!

MAKALA YA SPOTI: Qubaa Muslim yaibuka dume wa mashindano ya...

Afueni Arsenal baada ya Lacazette kuruhusiwa kucheza dhidi...

adminleo