• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 1:51 PM
SHANGAZI AKUJIBU: Nikishiriki tendo la ndoa naumwa na tumbo sana

SHANGAZI AKUJIBU: Nikishiriki tendo la ndoa naumwa na tumbo sana

Na SHANGAZI

KWAKO shangazi. Nimeolewa na tumejaliwa mtoto mmoja. Kuna jambo fulani kuhusu mwili wangu ambalo limeanza kunitia wasiwasi katika siku za hivi majuzi. Kila nikishiriki shughuli za chumbani na mume wangu huwa ninaumwa na tumbo kwa karibu wiki mbili mfululizo. Je, ni kwa nini?

Kupitia SMS

Mimi sina uwezo wa kukusaidia katika jambo kama hilo kwa sababu ni suala la kimatibabu ambalo linafaa kushughulikiwa na mtaalamu. Ushauri wangu ni kwamba umuone daktari mtaalamu wa masuala ya uzazi ili akusaidie.

 

Sina mtoto naye, nahisi ana kasoro

Kwako shangazi. Nimekuwa katika ndoa kwa miaka miwili sasa. Mume wangu aliponioa nilikuwa na mtoto kutokana na uhusiano wa awali. Katika miaka hiyo miwili tumejaribu kupata mtoto mwingine lakini hatujafaulu. Ninaamini kuwa mwenzangu ndiye mwenye kasoro. Ninaomba ushauri wako.

Kupitia SMS

Huwezi kuwa na hakika kuwa mume wako ndiye mwenye kasoro eti kwa kuwa wewe una mtoto uliyezaa na mwanamume mwingine. Sababu ni kuwa kasoro za kimwili zinaweza kumpata mtu wakati wowote. Ushauri wangu ni kuwa muende hospitalini mkapimwe ili mjue tatizo liko wapi na iwapo linaweza kutatuliwa.

 

Naogopa mabinti, nitampataje mke?

Shangazi mimi sijaoa na ninaogopa wanawake. Nifanyeje ili nipate mke?

Kupitia SMS

Sielewi ukimpata huyo mke utaishi naye namna gani kama unaogopa wanawake. Sina namna ya kukusaidia lakini nakufahamisha tu kwamba ukiendelea kuogopa wanawake hutawahi kuwa na mke maishani.

 

Ameanza kulala nje, nahofia anachepuka

Habari yako shangazi? Nimeolewa na tuna mtoto moja. Nampenda sana mume wangu na sijawahi kumshuku hata siku moja. Lakini siku za hivi majuzi amenishangaza sana kwa sababu ameanza kulala nje. Tabia yake hiyo inanitia hofu. Nahitaji ushauri wako.

Kupitia SMS

Kama hujamuuliza sababu yake kulala nje au mwenyewe kujieleza, sijui nitakusaidia vipi. Muulize usikie atasema nini, ukiridhika ni sawa, usiporidhika, uchukulie hizo kuwa dalili za mienendo isiyofaa na umwambie wazi kuwa huwezi kuivumilia.

 

Nimeoa tena na mke amtesa mwanangu

Habari zako shangazi? Nilikuwa nimeoa lakini mke wangu akaaga dunia miaka miwili iliyopita na kuniachia mtoto wetu wa pekee ambaye sasa ana miaka minane. Nilioa mke mwingine mwaka uliopita lakini ameanza kumtesa mtoto wangu. Nimemkanya na sasa anatishia kuniacha. Nishauri tafadhali.

Kupitia SMS

Ninaamini kwamba ulipomuoa mwanamke huyo ulimwambia ukweli kuwa una mtoto wa marehemu mke wako. Kwa sababu hiyo, kama kweli anakupenda anatarajiwa pia kumpenda mwanao. Mtoto wako ni damu yako na kwake kumtesa ni sawa tu na kukutesa wewe. Ni heri muachane kuliko kuendelea kuona mtoto wako akiteswa na mtu anayedai kuwa mke wako.

 

Amenifumania sasa anatisha kunibwaga

Vipi shangazi? Nilioa miaka mitano iliyopita na tuna watoto wawili. Ilifika wakati mama watoto akashindwa kunishibisha na nikalazimika kutafuta nje. Juzi alitufumania na sasa anatishia kuniacha. Nishauri.

Kupitia SMS

Ulipoamua kumuoa mke wako ulikuwa umetosheka kuwa ndiye anayekufaa. Lakini kutokana na tamaa, ukaona utafute kimada. Hayo ni masaibu ya kujitakia na ningekuwa yeye pia ningekuacha.

 

Tofauti kubwa kiumri inanitia wasiwasi

Hujambo shangazi? Nina umri wa miaka 26 na mwanamume mpenzi wangu ana umri wa miaka 42. Nampenda sana ingawa nahisi tofauti ya umri kati yetu ni kubwa sana. Nishauri.

Kupitia SMS

Mapenzi ya dhati hukiuka mipaka ya aina nyingi ikiwemo umri. Mahaba na mambo mengine yote yakiwa sawa, umri haufai kuwa hoja. Ondoa wasiwasi.

You can share this post!

MSHAIRI WETU: Boaz Aseli ‘Ustadh Kipepeo’

Mtihani mgumu kwa Ulinzi ikivaana na Tusker FC ligini

adminleo