• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 4:55 PM
SHANGAZI AKUJIBU: Mmoja wa wake wangu ametisha kuniacha

SHANGAZI AKUJIBU: Mmoja wa wake wangu ametisha kuniacha

Na SHANGAZI

HUJAMBO shangazi? Mimi nina wake wawili na ninawapenda wote. Hata hivyo, kuna mmoja wao anayenijali na kunipa raha zaidi kuliko mwenzake na nimejipata nikitumia muda wangu mwingi pamoja naye. Sasa mwenzake anatishia kuniacha akisema sina haja naye. Ukweli ni kuwa bado nampenda. Nishauri.

Kisa cha ndoa yako kinathibitisha kwamba mwanamume hawezi kuwapenda wanawake wawili kwa wakati mmoja na mara nyingi huvutiwa upande mmoja. Usimlaumu mwenzio kwa kulalamika na kutishia kujiondoa katika ndoa hiyo kwa sababu wewe ndiye umemuachia baridi. Tafuta namna ya kusawazisha mambo.

 

Amekana mimba ingawa ndiye wangu wa kwanza

Shikamoo shangazi? Nina umri wa miaka 21 na nimekuwa kwa uhusiano wa kimapenzi na mwanamume tunayefanya kazi pamoja. Nimepata mimba yake lakini ameikana akidai si yake ilhali ndiye mpenzi wangu wa kwanza na wa pekee. Naomba ushauri wako.

Hayo ndiyo matokeo ya mahusiano ya kimapenzi yasiyo na mpango. Kwa nini ukubali kupata mimba kutokana na uhusiano wa kimapenzi badala ya kusubiri ndoa? Ni wazi kuwa mpenzi wako hayuko tayari kuwajibika na ndiyo maana anakana mimba hiyo. Wakati mwingine utakumbuka kutumia kinga. Lakini kwa sasa jiandae kulea mtoto wako.

 

Alihepa aliponipa mimba, anitafuta

Kwako shangazi. Nilikuwa na uhusiano na mwanamume niliyempenda sana lakini akaniacha baada ya kunipa mimba. Baadaye nilimpata mwingine na akanioa. Sasa huyo wa awali amekuwa akinitumia jumbe za SMS kuniomba turudiane eti yuko tayari kunioa. Nishauri.

Huwezi kumwamini tena mtu kama huyo ambaye alikuacha wakati alipojua umebeba mimba yake. Isitoshe, unasema umeolewa na ninaamini umetulia katika ndoa. Mpuuze na uendelee na maisha yako.

 

Binti yangu aliye shule amepachikwa mimba

Kwako shangazi. Tafadhali ninahitaji ushauri wako. Kuna mwanamume ambaye amempa mimba binti yangu ambaye ni mwanafunzi wa shule ya upili. Nimejua kuhusu uhusiano wao majuzi tu na ninafikiria kumchukulia hatua. Nishauri.

Ni makosa kisheria kwa mtu yeyote kushiriki mapenzi na mwanafunzi hasa ambaye hajahitimu umri wa miaka 18. Iwapo unahisi hamuwezi kushauriana na kufikia maelewano na mwanamume huyo, una haki ya kumshtaki ili achukuliwe hatua.

 

Nilisafiri ng’ambo, nimepata mke ana mtoto wa mwingine

Vipi shangazi? Nilitumwa kazi ughaibuni na niliporudi nyumbani juzi nikapata mke wangu amezaa mtoto na mwanamume mwingine. Ninampenda sana na tumezaa watoto wawili pamoja. Nifanyeje?

Ingawa hujaelezea, inaonekana umekuwa nje kwa muda mrefu. Kuna uwezekano mkubwa mke wako hakufanya hivyo makusudi bali alizidiwa na upweke na hisia za kibinadamu akafanya makosa hayo. Unasema unampenda kwa hivyo jaribu kumsamehe.

 

Baba ya watoto wake amerudi

Shangazi hujambo? Nimekuwa na uhusiano wa miaka mitatu na mwanamke aliyeachana na mumewe na ana watoto watatu. Sasa baba ya watoto wake amerudi. Nishauri.

Kulingana na maelezo yako, mwanamke huyo na mume wake wameamua kurudiana. Kama ndivyo, huna budi kujiondoa kwani wenu umekuwa uhusiano tu wala hujamuoa. Sasa amekuwa tena mke wa mwenyewe na itakuwa haramu kuendelea na uhusiano huo.

 

Aliyenibaka ataka kuoa dada yangu

Kwako shangazi. Kuna mwanamume fulani ambaye alinibaka na sasa anataka kumuoa dada yangu. Je, niwatenganishe ama niachane nao? Tafadhali nishauri.

Kupitia SMS

Kama kweli mwanamume huyo alikubaka na ukaweka jambo hilo kuwa siri, huenda dada yako akose kukuamini na badala yake kudhani kuwa unamsingizia mchumba wake kusudi tu kuvunja uhusiano wao. Ni heri uachane nao.

You can share this post!

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Utulivu wa nafsi unakuhakikishia...

DOMO KAYA: Mbona 001 atukanganya?

adminleo