Jamvi La Siasa

Linda Mwananchi kuvamia ngome ya Matiang’i wiki ijayo

Na MWANDISHI WETU June 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 3

VUGUVUGU la Linda Mwananchi linatarajiwa kuingia katika maeneo ya Kisii na Nyamira wiki ijayo, hatua inayotafsiriwa na wachambuzi wa siasa kama jaribio la kupima ushawishi wa Dkt Fred Matiang’i katika ngome yake huku juhudi za kuunda muungano mkubwa wa upinzani zikizidi kushika kasi kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.
Hatua hiyo imejiri siku chache baada ya Dkt Matiang’i, ambaye amepitishwa na chama cha Jubilee kuwa mgombea wake wa urais, kufanya kikao na viongozi wa Linda Mwananchi akiwemo Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na Seneta wa Kisii Richard Onyonka.
Ingawa maudhui ya mkutano huo hayakuwekwa wazi, picha zilizochapishwa na Matiang’i kwenye mtandao wa X zimeimarisha uwezekano wa ushirikiano kati ya kundi ya Muungano wa Upinzani na vuguvugu la Linda Mwananchi.
Ziara ya Kisii na Nyamira inafanyika wakati ambapo eneo la Gusii limeibuka kuwa moja ya maeneo muhimu zaidi kisiasa nchini. Katika miezi ya hivi karibuni, Matiang’i ameendelea kuimarisha ushawishi wake nyumbani huku viongozi kadhaa wa eneo hilo wakijitokeza hadharani kumuunga mkono.
Nguvu zake zilidhihirika zaidi mwaka jana wakati wagombea waliokuwa wakimuunga mkono waliposhinda uchaguzi mdogo wa Nyamaiya, Nyansiongo na Ekerenyo katika Kaunti ya Nyamira, matokeo yaliyotikisa vyama vya ODM na UDA.
Kadiri mazungumzo ya kuunganisha upinzani yanavyoendelea, viongozi mbalimbali wamekuwa wakisisitiza umuhimu wa kuwa na mgombea mmoja wa kumenyana na Rais William Ruto mwaka 2027.
Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna ambaye ni kinara wa Linda Mwananchi alisema hakuna njia nyingine ya kumshinda Ruto isipokuwa upinzani kuungana.
“Hakuna fomula nyingine. Mbele ya Mungu hakuna fomula nyingine isipokuwa tiketi moja dhidi ya William Ruto,” alisema Sifuna.
Kwa upande wake, aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua amekuwa akisisitiza kuwa kila kiongozi wa upinzani lazima kwanza aimarishe ngome yake kabla ya kuingia katika mazungumzo ya kugawana nafasi za kitaifa.
Wakazi Mlima waheshimu Matiang’i
“Mimi nataka tukubaliane; ndio mimi niende nitembeze Matiang’i Mlimani. Ili watu wa Mlima wamheshimu lazima kwanza aheshimike hapa nyumbani,” alisema Gachagua katika mkutano wa awali wa viongozi wa upinzani.
Kauli hiyo inaonyesha umuhimu wa eneo la Gusii katika hesabu za kisiasa za mwaka 2027. Wanasiasa wengi wanaamini kuwa uwezo wa Matiang’i kudhibiti kura za nyumbani utakuwa msingi wa nguvu zake katika mazungumzo ya kuunda muungano wa upinzani.
Hata hivyo, washirika wa Rais Ruto wameendelea kupigania ushawishi katika eneo hilo. Gavana wa Kisii Simba Arati, Waziri wa Elimu Julius Ogamba na Mbunge wa South Mugirango Silvanus Osoro wamekuwa mstari wa mbele kuhamasisha uungwaji mkono kwa muhula wa pili wa Rais Ruto.
Lakini mikutano ya hivi karibuni ya upinzani imevutia umati mkubwa wa wananchi, jambo linaloashiria kuwa ushindani wa kisiasa katika eneo la Gusii unaendelea kushamiri.
Ziara ya Linda Mwananchi katika Kisii na Nyamira sasa inatarajiwa kumtia nguvu zaidi Matiang’i katika eneo lake la nyumbani na uwezo wa upinzani kuunganisha nguvu zake dhidi ya Kenya Kwanza.
Iwapo mwelekeo wa sasa utaendelea, eneo la Gusii linaweza kuwa mojawapo ya maeneo yatakayoamua mwelekeo wa siasa za Kenya katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.
Ni katika muktadha huo ambapo wachambuzi wanasema Matiang’i alikutana na Linda Mwananchi kabla ya ziara ya vuguvugu hilo katika eneo la Gusii—Kaunti za Kisii na Nyamira—ambako limepanga mikutano ya kisiasa Juni 26, 2026, ikiwa ni sehemu ya kampeni za kuimarisha ushawishi wake kabla ya uchaguzi.
Ziara hiyo inaweza kuongeza ushawishi wa Matiang’i katika eneo lake la asili, ambalo limekuwa likibadilika kwa kasi kisiasa. Gusii kwa muda mrefu ilikuwa ngome ya ODM, huku UDA pia ikihifadhi ushawishi wake, lakini hali sasa inaonekana kubadilika.
Kwa mujibu wa wachambuzi wa siasa, mkutano wa Matiang’i na timu ya Linda Mwananchi ni sehemu ya mkakati mpana wa kupanga safu ya upinzani kabla ya mazungumzo ya kitaifa ya kugawana madaraka.
Tayari tafiti mbalimbali, ikiwemo za TIFA, zinaonyesha uwezekano wa ushirikiano mpya ndani ya upinzani, huku majina kama Kalonzo Musyoka, Matiangi na Sifuna yakitajwa.