• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 6:55 PM
Genge la Gaza lavamia na kuhangaisha Tana River

Genge la Gaza lavamia na kuhangaisha Tana River

Na STEPHEN ODUOR

KWA mwezi mmoja sasa, kundi la watoto wa chini ya zaidi ya miaka 16 linaendelea kuhangaisha wakazi wa eneo la Madogo, kaunti ya Tana River.

Vijana hao zaidi ya kumi hudhuru watu kutumia visu na silaha nyingine mbali na kuwapora mali zao.

Jina Gaza, limewatia wengi uoga, kwani, vijana hao sasa wameuteka mji na kuufanya himaya yao ya uhalifu na kutekelezea unyama wao.

Anne Mukami anakumbuka wazi jinsi alivyoibiwa pesa na vijana hao,pale alipokuwa ametoka katika pilkapilka za kuchuma mjini Garissa.

“Nilikuwa na kama shilingi elfu sitini na tano hivi, na nilikuwa nimepangia kulipia mali hiyo kesho, sasa tuliposimama na yule mtu wa bodaboda kwa hiyo duka wakatokea vijana saba, mmoja alikuwa na kitu kama bunduki kwa kiuno, hao wengine walikuwa na visu na panga kali, wakaniambia niwape kila kitu mpaka lesso na mtandio,” alisimulia.

Hata baada ya kumuibia vijana wale hawakuwa wamekamilisha biashara yao, kwani watatu kati yao waliabiri pikipiki aliyokuwa ameletwa nayo baada ya kumpora hata dereva, huku wanne kati ya vijana wale wakimsindikiza Bi Mukami hadi mlangoni pake na kumuonya dhidi ya kuripoti kisa hicho kwa polisi. .

Walihakikisha ameingia kwake na kumpa onyo dhidi ya kupiga ukemi wa kuwaamsha majirani, la sivyo wangemchoma ndani ya nyumba.

Bi Mukami alimalizia uchungu wake kwa machozi ndani ya nyumba, na kukataa uamuzi wa kuuhama mji na kuelekea Garissa jua litakapochomoza.

Asubuhi ile alipata taarifa ya kuwa aliyekuwa dereva wa pikipiki alivuliwa nguo na kuachwa uchi wa mnyama baada ya kutiwa alama za kisu, hata baada ya kuwafikisha walikokuwa wakienda,na baadaye kuambiwa asisimame popote isipokuwa kwake.

“Walimwambia kuwa tayari washamtia alama za Gaza, kuwa hawatamwibia tena ila wakimhitaji kwa shughuli yoyote watatafuta huduma zake.

Ilibainika kuwa baadhi ya waathiriwa wa genge hili walikuwa na alama za visu kwa mtindo flani,huku wale wanaosumbua wanapoporwa hudungwa visu na kuachwa na majeraha mabaya.

Wanaotiwa alama hupewa onyo dhidi ya kuwaonyesha watu alama hizo,huku wakiekwa chini ya ulinzi wa watu wasiowajua katika maenoe yao ya kazi.

Kulingana na wakaazi,kadri siku zinavyokwenda,kundi hilo linazidi kuwa kubwa na jinamaizi hatari katika jamii,kwani,vijana tayari wanadondoka shuleni na kujipata katika makundi hayo.

Kwa vijana walio katika maeneo ya kazi haswa wanawake,wamelezimishwa kutoa ada ya shilingi elfu moja kwa kundi hilo,pesa zinazokusanywa ghafla kila mwisho wa mwezi, pasi na kujua wasaa wala dakika.

Ada hiyo huchukuliwa kwa ajili ya kuwalinda na kama Ishara ya kusalimu amri,lasivyo mja hukosa amani kwa kuporwa na kupigwa ngeta kila siku, na wakati mwngine huibiwa kila kitu nyumbani na kuachiwa sakafu wazi.

Zainab Hawa amekuwa akilipa ada yake ya shilingi elfu moja kila mwezi tangu anusurike kifo alipokpiga ukemi katika pilkapilka za kuibiwa.

“Watagonga mlango hata saa nane asubuhi, ama labda waje katika maeneo yako ya kazi ama wakutane nawe kanisani,hutajua kama wanakuja, na hutamjua ni nani kaja,utaskia tu dogo flani kanisani hapo kando yako ywakwambia redeem bonga points ama nipe sadaka ya mwezi,hapo utajua tayari ni wao maana,”alisimulia.

Iwapo anayedaiwa hana pesa atembeapo, huambiwa kuzifikisha mahali flani kwa mdaiwa mwenzake, au labda kuviweka katika kituo flani ambapo pindi zinapopokewa mambo hutulia kwake.

Vijana hao hawapendi kutumia simu kuchukua ada,na huwa katili kwa yeyote anayekiuka ulipaji wa ada hiyo.

You can share this post!

Tafadhali punguza kasi ya utekelezaji mtaala mpya, Magoha...

Waathiriwa wa 2007/8 kortini kutolipwa fidia baada ya...

adminleo