• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 9:12 AM
Visiki vizito katika azma ya Jubilee kufanya uchaguzi

Visiki vizito katika azma ya Jubilee kufanya uchaguzi

Na WANJOHI GITHAE na BENSON MATHEKA

CHAMA cha Jubilee kinakabiliwa na kibarua kigumu zaidi kinapojiandaa kwa uchaguzi kote nchini huku wafuasi wa Naibu Rais wakilalamika kuwa kuna njama ya kuwafungia kugombea nyadhifa za uongozi.

Kulingana na katiba ya chama hicho, uchaguzi unafaa kufanyika Machi 2020.

Maafisa wa chama hicho walifahamisha Taifa Leo kwamba Baraza Kuu la Kitaifa (NEC) litakutana hivi karibuni kuweka mikakati ya uchaguzi ambayo wanachama wanapaswa kufuata.

Kulingana na katiba ya Jubilee, uchaguzi unapaswa kuanzia mashinani hadi kongamano la kitaifa la wajumbe ambapo maafisa wa kitaifa watachaguliwa.

Kwa wakati huu, chama hicho kimegawanyika katika makundi mawili; ‘Tangatanga’ linalomuunga Dkt Ruto na ‘Kieleweke’ linalopinga azma yake ya kugombea urais.

Chama hicho kinakabiliwa na msukosuko ambao baadhi ya wanachama wanasema unachangiwa na viongozi kutokutana kuzungumza kwa sauti moja.

Dkt Ruto amekuwa akitengwa serikalini na wandani wake wa kisiasa wanadai kwamba wanahangaishwa na serikali. Wiki hii, Rais Kenyatta alitoa tamko la wazi kuashiria kwamba hatamuunga mkono kuwa mrithi wake kwenye uchaguzi mkuu ujao aliposema ni Mungu anayejua atakayechaguliwa Rais.

Naibu rais ameendelea na kampeni zake na amekuwa akiashiria kwamba anafahamu kuna njama za kumzuia kuwa rais kupitia uchaguzi wa chama.

Uchaguzi wa Jubilee unafuatiliwa kwa karibu na wanachama wa mirengo yote miwili ‘Kieleweke’ na ‘Tangatanga’ ambao wameapa kutohama chama hicho.

Wanachama wa Kieleweke wamekuwa wakipendekeza kuwa viongozi waliochaguliwa wasiwanie nyadhifa za uongozi wa chama, msimamo ambao Tangatanga inapinga.

Kulingana na Tangatanga, wabunge wa zamani wanataka kuchukua nyadhifa za uongozi chamani ili wamzime Ruto na wafuasi wake kwenye uteuzi wa wagombeaji wa uchaguzi mkuu wa 2022.

Hivi majuzi, chama hicho kilipokea Sh190 milioni ambazo Katibu Mkuu Raphael Tuju anasema zitatumiwa kuandaa uchaguzi.

Bw Tuju ambaye majuzi alishambuliwa na wafuasi wa Dkt Ruto wakitaka atimuliwe alisema maandalizi ya uchaguzi yanaendelea.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa wanaowania nyadhifa za uongozi lazima wahudhurie mafunzo kwanza ili waelewe malengo yake.

“Hakuna atakayeruhusiwa kugombea wadhifa ikiwa anaendeleza chuki za kikabila. Malengo ya chama ni umoja wa kitaifa,” alisema.

Alisema ni lazima viongozi wote waliochaguliwa na wanachama wanaowania nyadhifa chamani wahudhurie mafunzo hayo.

“Warsha hizo zitakuwa sehemu ya maandalizi ya uchaguzi,” alisema na kuongeza kuwa watawasajili wanachama kabla ya uchaguzi.

Maafisa wapya

Naibu katibu mkuu wa chama hicho Caleb Kositany alisema ni lazima kiwe na maafisa wapya kufikia Machi 2020 ili kijiandae kumteua mgombea urais 2021.

“NEC itakutana hivi karibuni kujadili na kutoa mwelekeo,” alisema.

Uchaguzi huo unaandaliwa huku Rais Uhuru Kenyatta ambaye ni kiongozi wa Jubilee Party akipuuza miito ya ‘Tangatanga’ ya kuitisha kikao cha wabunge.

Bw Tuju alikiri kwamba chama hicho kitakabiliwa na changamoto katika kuandaa uchaguzi huo.

You can share this post!

Kenya Simbas yafanya Zambia kitoweo Victoria Cup

KINAYA: Punguza Mizigo, Kujenga Daraja hazina tofauti,...

adminleo