• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
Raila anamwadhibu Wetang’ula kwa kususia ‘kiapo’, asema mbunge

Raila anamwadhibu Wetang’ula kwa kususia ‘kiapo’, asema mbunge

Na CHARLES WASONGA

MBUNGE mmoja wa Ford Kenya ameelekeza kidole cha lawama kwa kiongozi wa ODM Raila Odinga kufuatia kuondolewa kwa Moses Wetang’ula kama kiongozi wa wachache katika seneti.

Bw Vincent Kemusi Magaka (pichani juu) ambaye ni mbunge wa Mugirango Magharibi  Jumatano alidai Bw Odinga ndiye alitoa idhini kwa maseneta wa ODM, walio wengi, kuchukua hatua hiyo kama njia ya kulipisha kisasi kufuatia hatua ya Wetang’ula na wenzake wawili kufeli kuhudhuria sherehe ya “kuapishwa” kwake katika bustani ya Uhuru, Nairobi.

“Raila alikuwa akilipisha kisasi dhidi ya Wetang’ula kwa kutohudhuria ile halfla ya Uhuru Park. Hii ndio maana aliwashauri maseneta 20 wa ODM kupiga kura na kumwondoa kiongozi wa chama changu,” akasema  kwenye kikao na wanahabari katika majengo ya Bunge, Nairobi.

Bw Mogaka alisema kufuatia hatua hiyo, vinara watatu wa NASA, Musalia Mudavadi (ANC), Kalonzo Musyoka (Wiper) na Wetang’ula watakutana juma lijalo kupanga mkakati wa kufurusha ODM kutoka Muungano wa NASA.

“Hatuwezi kuendelea kushirikiana na watu ambao wanalenga kuporomosha muungano. Hatutawavumilia watu wenye kiburi na wanaolenga kuhujumu vinara wa NASA.

Ni heri kusalie na wabunge wachache katika upinzani lakini wawe ni wale ambao wataendelea kuikosoa serikali  iliyoko mamlakani,” akasema huku akitoa mfano wa Afrika  Kusini ambapo chama cha Julius Malema chenye wabunge 17 kilichochea kung’olewa mamlakani kwa Rais wa zamani Jacob Zuma.

You can share this post!

Kwa kila bao atakalofunga Salah, tutawapa wateja wetu...

Jubilee yakiri Cambridge Analytica iliwasaidia uchaguzini...

adminleo