• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
Magoha adinda kutetea wanavyuo wanaokosa hafla

Magoha adinda kutetea wanavyuo wanaokosa hafla

Na WINNIE ATIENO

WAZIRI wa Elimu, Prof George Magoha ametetea wahadhiri wa vyuo vikuu kwa kuondoa wanafunzi ambao hawajafuzu wasishiriki kwenye mahafali.

Kumekuwa na malalamishi kutoka kwa wanafunzi wa vyuo mbalimbali kwamba wahadhiri huwafanya kukosa kufuzu kutoka vyuoni kwa sababu zisizo na msingi.

Chuo Kikuu cha Moi ndicho kimeibuka kuwa na malalamishi mengi zaidi ya aina hii, ikiwemo majuzi ambapo mamia ya wanafunzi waliokuwa wanatarajia kushiriki kwenye mahafali walikuta hawamo kwenye orodha.

Ijumaa, chama cha wanafunzi (KUSO) kilitishia kwenda mahakamani kushtaki chuo kikuu cha Moi baada ya wanafunzi 700 kukosekana kwenye orodha hiyo huku wenzao wakiwa wanatarajiwa kufuzu mnamo Alhamisi wiki hii.

Jana, Prof Magoha alisema wahadhiri wana mamlaka ya kuamua iwapo mwanafunzi amehitimu kufuzu au la.

“Tunakaa kana kwamba nia yetu kuu ni kuwapa wanafunzi vyeti. Hivi sasa kuna wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Moi ambao wanalalamika kuwa majina yao hayamo kwenye orodha ya mahafala. Suala muhimu si la jina lako kuwa kwenye orodha, hii inahusu mhadhiri wako kutosheka kwamba umepata ujuzi wa kutosha ili ufuzu,” akasema Prof Magoha.

Aliwataka wakufunzi wawe na ujasiri wa kuwaambia wanafunzi kwamba hawatafuzu kwa ajili ya suala hili au lile.

Wakati huo huo, wizara ya elimu imetangaza kuwa muundo wa mtaala utakaoongoza mafunzo katika taasisi za mafunzo ya walimu kuhusu mtaala mpya utakuwa tayari kati ya wiki tatu na miezi mitano ijayo.

Akizungumza katika uzinduzi rasmi wa warsha ya chama cha walimu wakuu wa vyuo vya elimu nchini inayoendelea katika hoteli ya Travellers mjini Mombasa, Prof Magoha aliwashauri walimu hao kutia bidii katika kuelimisha walimu watarajiwa mtaala huo.

“Ili kuwaelimisha watoto wetu kutumia mfumo mpya mnapaswa kwanza kuelewa nini kinahitajika kabla yenu kupitisha ujuzi huo kwa walimu ambao watafundisha madarasani,”alisema.

Zaidi ya walimu wakuu 300 kutoka kwa vyuo vya serikali na vile vya kibinafsi, chama cha walimu,Taasisi ya kushughulikia mtaala walikongamana Mombasa kwa kusudi la kuangazia mtaala mpya.

Waziri huyo aliwashauri walimu kujivunia kazi wanayoifanya.

“Najivunia kuwa mwalimu kwa sababu ya watu wengi wakubwa kama madaktari wa upasuaji waliopitia mikononi mwangu. Wananitambua kuwa mimi si mtu rahisi lakini wanajuwa kuwa ni ugumu wangu uliowafanya wao kufaulu katika masomo yao,” akasema.

Kongamano hilo ambalo ni la nane mada yake ikiwa kuboresha mwalimu wa karne ya 21, linapanga kuangazia masuala ibuka katika mafunzo ya walimu katika mtaala mpya.

Mwenyekiti wa chama cha vyuo vikuu, Bw Barasa Wafula alisema kongamano hilo limefanyika wakati muafaka ambapo serikali imeanzisha mtaala mpya.

Muungano huo pia ulihakikishia serikali kuwa utaiunga mkono katika kutekeleza mfumo mpya wa elimu.

Aliomba serikali kuajiri walimu zaidi ili wanafunzi wapokee elimu bora.

Vilevile, Bw Wafula alisisitiza kuwa ni muhimu walimu wanaofanya diploma kupokea mafunzo ya mtaala mpya ili wawe tayari kuyatumia.

You can share this post!

Kaunti yatakiwa kubuni sera ya kupunguza chokoraa jijini

Raha kijijini baada ya baba kumuua mwanawe!

adminleo