• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Ziara ya Rais Uhuru na Raila mjini Kisumu yaahirishwa

Ziara ya Rais Uhuru na Raila mjini Kisumu yaahirishwa

Na JUSTUS WANGA

MKUTANO wa pamoja kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa NASA Raila Odinga uliotaribiwa kufanyika wiki hii mjini Kisumu umeahirishwa kutoa nafasi kwa muda wa kushughulikia masuala ibuka yanayotisha kuathiri muafaka kati yao.

Wandani wa Bw Odinga wameanza kushuku kujitolea kwa Jubilee katika mchakato wa mazungumzo baada ya kiongozi wa wengine bunge Aden Duale kupinga kujumuishwa kwa suala ya mageuzi  katika mfumo wa uchaguzi ambalo ni mojawapo yale ambayo Rais na Odinga walikubali kujadili.

Akiongea katika runinga moja ya humu nchini Bw Duale ambaye ni Mbunge wa Garissa Mjini pia alipuuzilia mbali mageuzi katika mfumo wa uongozi nchini.

Wakati huo huo, mpango wa balozi Martin Kimani na Wakili Paul Mwangi kuwahutubia wanahabari Ijumaa ili kuelezea hatua iliyopigwa kuhusu suala hilo iliahirishwa dakika zake mwisho.

Mbw Kimani na Mwangi waliteuliwa na Rais Kenyatta pamoja na Bw Odinga kutayarisha mwongozo ambao utasaidia kufanikisha malengo ya mwafaka huo.
Duru zilisema kuwa “kuna masuala ambayo pande husika hawajakubaliana.” Walipofikiwa kwa njia ya siku wawili hao hawakutaja sababu ya kufutilia mbali kikao na wanahabari.

Taifa Jumapili pia imegundua kuwa Kamati hiyo itapanuliwa kwa kujumuisha angalau wanachama watano kutoka kila upande huku akianza kibarua rasmi.

Shauku ya kambi ya Bw Odinga inatokana na hali kwamba japo ameshawishi uongozi wa chama hicho kuunga mkono ushirikiano huo, kufikia sasa Rais Kenyatta hajaitisha mkutano wa kundi la wabunge wake (PG) au asasi yoyote ya chama hicho kuhimiza wafuasi wake kuunga mkono mwafaka huo. Vile vile, wanasema Rais Kenyatta hajaitisha kikao maalum cha baraza la mawaziri kuwajuza kuhusu yaliyomo ndani ya mkataba kati yake na Bw Odinga.

“Tunataka kuona taarifa kutoka afisi ya Rais ikielezea hatua ambazo zimewekwa kuafikia uwiano na masuala ambayo yalikubaliwa. Sawa na Odinga, tunaamini kwamba Rais ana nia njema. Tunataka kuona wakianza kazi,” mmoja wa wandani wa Bw Odinga alisema.

Chama cha ODM kinashikilia kuwa hatima ya mwafaka huo utategemea kama iwapo Rais alielekeza nchini kufunua ukurasa mpya huku masuala ya serikali yakiendeshwa kwa namna tofauti.

Hata hivyo, hakuna kiongozi kutoka kambi ya Kenyatta ambaye amepinga mwafaka huo isipokuwa Seneta wa Tharaka Nithi Profesa Kithure Kindiki ambaye ameonya Rais kutahadhari anapojadiliana na Bw Odinga kwa sababu, “ni mwanasiasa mjanja”.

Seneta wa Siaya James Orengo, ambaye ni mshirika wa karibu wa Bw Odinga aliwaonya Rais Kenyatta na kiongozi huo wa upinzani kuwaonya wafuasi wao dhidi ya kutoa matamshi ambayo yanaweza kusambaratisha mwafaka huo.

 

You can share this post!

Niliporwa mamilioni niliyochangiwa na Wakenya –...

Wavuvi wa Kenya wavamiwa tena na polisi wa Uganda

adminleo