• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Jirongo asimulia Raila alivyomsaidia kupata kazi Tanzania

Jirongo asimulia Raila alivyomsaidia kupata kazi Tanzania

Bw Cyrus Jirongo akihutubu awali. Picha/ Maktaba

Na BARACK ODUOR

ALIYEKUWA mgombeaji urais Cyrus Jirongo amempongeza kiongozi wa NASA Raila Odinga kwa kumsaidia na kumwezesha kupata ajira. Jirongo ambaye ni Mbunge wa zamani wa Lugari alidai kuwa Rais Uhuru Kenyatta na Naibu wake William Ruto walimtelekeza.

Mwanasiasa huyo alidai viongozi hao wawili wa Jubilee, ambao wamekuwa wandani wake, walimpuuzilia alipowageukia akitaka wamsaidie.

“Nitaendelea kuwa kushirikiana na jamii ya Waluo kwa sasa hata juzi nilimtembelea Bw Odinga na nikamwelezea jinsi viongozi wakuu wa Jubilee wamenitelekeza,” akasema Bw Jirongo.

Akiongea wakati wa mazishi ya Mama Julia Amayo, mkewe aliyekuwa Mbunge wa Karachuonyo Okiki Amayo, Jirongo alifichua jinsi alivyosafirishwa na Bw Odinga hadi Tanzania ambapo kiongozi huyo wa NASA alimfahamisha kwa Rais John Magufuli.

“Ni Bw Odinga alinisaidia kwa kunijulisha kwa Rais wa Tanzania na Waziri Mkuu wa nchi hiyo ambaye baadaye alinipa kazi,” Bw Jirongo akawaambia waombolezaji katika kijiji cha Kakdhimu, eneo bunge la Karanchuonyo, kaunti ya Homa Bay.

Ingawa hakufichua ni kazi gani alipewa, alisema anamshukuru Bw Odinga na kuunga mkono mwafaka kati yake na Rais Kenyatta.

“Naunga mkono ushirikiano kati ya Odinga na Rais Kenyatta kwani nafahamu utaleta manufaa makubwa kwa Wakenya wote,” akasema.

Bw Jirongo alisema Odinga sasa anafaa kupewa heshima na wanasiasa wa mirengo ya Jubilee na NASA kutokana na hatua yake ya kuanzisha mazungumzo kwa ajili ya kuunganisha nchi.

Naye aliyekuwa Mbunge wa Rangwe Shem Ochuodho alipongeza ushirikiano kati ya viongozi hao wawili lakini akawataka kuutumia kuunganisha nchini.

“Mazungumzo kati ya Kiongozi wa NASA Raila Odinga na Rais Kenyatta yanafaa kuwa zaidi ya salama ya mkono ili yaweze kuafaidi Wakenya,” akasema Bw Ochuodho ambaye pia ndiye Mwenyekiti wa Wakenya wanaoishi Ughaibuni.

Aliwataka wanasiasa nchini kuepukana na siasa za migawanyiko bali waungane na viongozi hao wawili kuleta maridhiano nchini baada ya kukamilika kwa kipindi cha uchaguzi.

“Wanasiasa wote nchini hawana jingine ila kuwaunga mkono Rais Kenyatta na Odinga katika mchakato wa kuleta maridhiano miongoni kwa Wakenya,” akasema.

Viongozi wengine waliohudhuria mazishi hayo ni pamoja na Gavana wa Homa Baye Cypria Awiti, aliyekuwa Mbunge wa Rangwe Philip Okundi, kati ya wengine.

You can share this post!

Kalonzo aandaliwa kuwarithi Uhuru na Raila

JAMVI: Uhuru afanikiwa kupunguza makali ya vinara wa...

adminleo