• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
Trump taabani huku spika akiidhinisha achunguzwe

Trump taabani huku spika akiidhinisha achunguzwe

Na AFP

SPIKA wa Bunge la Amerika, Nancy Pelosi ameagiza kuanzishwa kwa harakati za kutaka kumng’oa ofisini Rais Donald Trump kutokana na madai ya kutumia mamlaka yake vibaya.

Inadaiwa kwamba, Rais Trump ameunda njama ya kutaka kumaliza wapinzani wake wa kisiasa kwa kushirikiana na serikali ya Ukraine.

Taarifa zasema Rais Trump alimshinikiza Rais wa Ukraine kuanzisha uchunguzi dhidi ya aliyekuwa makamu wa Rais Joe Biden ili kumwezesha kutumia sakata hiyo katika kampeni zake za urais 2020.

Biden ambaye alikuwa naibu wa rais wa Barack Obama, tayari ametangaza kuwania urais kupitia chama cha Democratic na anapigiwa upato wa kumto kijasho Trump katika uchaguzi mkuu ujao.

Spika Pelosi alisema Trump ni sharti awajibishwe.

Kiongozi huyo wa Amerika, hata hivyo, amepuuzilia mbali madai hayo akisema anawindwa na mahasimu wake wa kisiasa.

Wabunge wengi wanaunga kutimuliwa kwa Rais Trump lakini hoja hiyo huenda ikagonga mwamba katika Seneti kwani wengi wa maseneta ni wa chama tawala cha Republican.

Rais Trump ameahidi kuchapisha mambo aliyozungumza na kiongozi wa Ukraine kwa njia ya simu.

Endapo hoja ya kumtimua Trump itapitishwa, basi kiongozi huyo wa chama cha Republican atakuwa rais wa tatu kung’olewa mamlakani katika historia ya Amerika.

Idadi ya wabunge, maseneta

Chama cha upinzani cha Democratic kina idadi kubwa ya wabunge lakini kina maseneta wachache.

Hiyo inamaanisha kuwa huenda ikawa vigumu kwa hoja hiyo kupitishwa katika Seneti.

Pelosi amekuwa akishinikizwa kuidhinisha uchunguzi utakaosababisha Trump kung’olewa mamlakani kufuatia madai ya kutumia mamlaka yake kumshinikiza Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky kuanzisha uchunguzi dhidi ya Biden.

Inadaiwa kwamba, Rais Trump alimtaka Rais Zelensky kuanzisha uchunguzi dhidi ya Biden kuhusu sakata ya ufisadi ndiposa apatie nchi hiyo msaada wa kijeshi.

Rais Trump amekiri kujadili Joe Biden katika mazungumzo yake na Rais Zelensky mnamo Julai 25 lakini amekanusha madai kuwa alitaka mwanasiasa huyo wa chama cha Democratic achunguzwe.

Marais wawili ambao bunge limewahi kupitisha kura ya kuwang’oa afisini ni Andrew Johnson (1868) na Bill Clinton (1998). Wawili hao, hata hivyo, walinusuriwa na Seneti.

Richard Nixon alijiuzulu mnamo Agosti 1974 kabla ya wabunge kumng’oa kutoka afisini.

You can share this post!

Raila akosa kufaulu kumtimua Chebukati na wenzake wawili

KIU YA UFANISI: Mradi wa maziwa unaonawiri na kunufaisha...

adminleo