• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:39 PM
Chipu yabandua Madagascar kutinga fainali Namibia

Chipu yabandua Madagascar kutinga fainali Namibia

Na GEOFFREY ANENE

CHIPU ya Kenya imetinga fainali ya mashindano ya raga ya Bara Afrika ya ukanda wa Afrika ya Kusini baada ya kulipua Madagascar 51-13 katika nusu-fainali ya kwanza uwanjani Hage Geingob jijini Windhoek, Namibia, Machi 28, 2018.

Vijana wa kocha Paul Odera watakabiliana na mabingwa mara nane Namibia, ambao wameshinda mataji sita yaliyopita, katika fainali hapo Machi 31.

Nahodha Xavier Kipng’etich (no. 9) atambulisha wachezaji wa Chipu kabla ya Kenya kuvaana na Madagascar. Picha/ Hisani

Namibia walitolewa kijasho kabla ya kujikatia tiketi ya kushiriki fainali kwa kulima majirani Zimbabwe 27-17 katika nusu-fainali ya pili uwanjani humu.

Mshindi kati ya Kenya na Namibia atamenyana na mshindi wa Afrika ya Kaskazini kati ya Tunisia na Senegal. Bingwa wa Afrika ataingia mashindano ya dunia ya Junior World Rugby Trophy (JWRT) baadaye mwaka huu.

Chipu na Namibia zikimenyana katika fainali ya mwaka 2017. Picha/ Hisani

Chipu, ambayo iliongoza 24-10 wakati wa mapumziko, ililemea Madagascar kupitia alama za Mark Mutuku (miguso miwili), Xavier Kipng’etich (mikwaju mitatu, miguso miwili na penalti moja), Victor Matiko (mguso na mkwaju), Joshua Macharia (mikwaju miwili) na Monate Akuei na Jeff Mutuku (mguso mmoja kila mmoja) na penalti moja. Madagascar ilifunga penalti mbili na mguso mmoja.

Mechi za Afrika ya Kaskazini, ambazo ziliandaliwa mjini Monastir nchini Tunisia mnamo Machi 28, zilishuhudia Senegal ikibwaga Morocco 30-25 nayo Tunisia ikakung’uta Ivory Coast 15-11.

You can share this post!

NDIVYO SIVYO: ‘Makanga’ au ‘manamba’ hayafai katika...

Makocha wa timu za raga Kenya watangaza vikosi vya Hong...

adminleo