• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 5:55 AM
LSK yakerwa na mazoea ya maafisa wa serikali kudharau sheria

LSK yakerwa na mazoea ya maafisa wa serikali kudharau sheria

Na BENSON MATHEKA
CHAMA cha Wanasheria Kenya (LSK), Alhamisi kilisikitishwa na hatua ya maafisa wa  serikali ya kudharau na kupuuza maagizo ya mahakama na kushambuliwa kwa mawakili wakitekeleza kazi yao.

Chama hicho kimesema kwamba katiba inasisitiza kuwa mahakama zinapatiwa mamlaka na raia sawa na serikali kuu na bunge na maagizo ya majaji yanafaa kuheshimiwa.

Naibu Mwenyekiti wa LSK, Bi Harieti Chiggai alisema maafisa wa serikali wanafaa kuheshimu maagizo ya mahakama wanavyoheshimu sheria zinazotungwa na kupitishwa na bunge kama njia ya pekee ya kuimarisha utawala wa sheria.

“Idara zote zilizobuniwa chini ya katiba, ni lazima ziheshimu katiba na sio moja kuhujumu nyingine,” alisema Bi Chiggai akisoma taarifa ya pamoja ya chama hicho, Tume ya Taifa ya Haki za Binadamu na Baraza la Wanahabari kuhusu kuhangaishwa kwa wakili Miguna Miguna.

Maafisa wa serikali walikataa kutii maagizo zaidi ya 10 ambayo mahakama ilitoa kuhusiana na masaibu ya Bw Miguna tangu wakili huyo alipokamatwa kwa kumuapisha kinara wa NASA Raila Odinga kuwa “rais wa wananchi.”

“Hakuna mtu au shirika lolote, iwe katika serikali au shirika la kibinafsi ana uhuru wa kuchagua maagizo anayopaswa kuheshimu. Na ikiwa serikali haikubaliani na agizo lolote, kuna utaratibu wa kutaka lisimamishwe au kukata rufaa. Tunaomba serikali kuonyesha mfano mwema wa kufuata utawala wa sheria na kwa kuheshimu katiba,” alisema.

LSK inamtaka Rais Uhuru Kenyatta kuonyesha kujitolea kwake kuunganisha nchi alipoahidi kwenye mwafaka wake na kiongozi wa NASA Raila Odinga kwa kuagiza Bw Miguna kurudi Kenya.

“Tunaiomba serikali kushughulikia kwa haraka hali ya Bw Miguna kwa utaalamu wa hali ya juu na kuepuka aibu ambayo tunashuhudia,” alisema.

Chama hicho kinaitaka serikali kutowazuia mawakili kufanya kazi yao. Mnamo Jumatano usiku mawakili James Orengo, Nelson Havi na Julie Soweto walizuiwa na polisi kuwakabadhi maafisa wa uhamiaji katika uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Jomo Kenyatta (JKIA), agizo la kuwataka wasimfurushe Bw Miguna.

“Tunaomba serikali kuwaruhusu mawakili kutekeleza majukumu yao halali bila kuwekewa vizingiti,” alisema Bi Chiggai.

You can share this post!

Gor yakanusha kutowalipa wachezaji licha ya kutatizika...

Ni aibu kwa serikali kumnyanyasa raia aliyezaliwa Kenya...

adminleo