• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
AKILIJIBU: Ningependa kuelimishwa kuhusu umuhimu wa kula karoti

AKILIJIBU: Ningependa kuelimishwa kuhusu umuhimu wa kula karoti

Na CHRIS ADUNGO

SWALI: Jina langu ni Rebecca Sanya kutoka Soy. Nimekuwa mkulima wa karoti kwa muda sasa. Ingawa hivyo, wingi wa zao hili kwa sasa katika eneo hili limevuruga biashara. Ili niuze, yanibidi kutoa maelezo marefu kwa wateja wangu kuhusu manufaa ya karoti. Naogopa kuwapotosha. Je, karoti zina umuhimu gani?

JIBU: Asilimia kubwa ya watu hupenda kutumia karoti kama kiungo katika mboga au kitoweo, na si kuila karoti ikiwa mbichi. Wataalamu wanashauri kwamba ili uwe na afya bora, unatakiwa ule angalau karoti sita kwa wiki au moja kwa siku. Unaweza kula karoti ya kuchemsha, kunywa juisi yake au hata kula ikiwa mbichi.

Faida za kula karoti ni nyingi. Karoti husaidia kuimarisha macho kuona vizuri, mfano tatizo la kutoona vizuri usiku. Pia inasaidia kuondoa matatizo ya mzio (allergy) kwenye macho, mfano macho kuwasha kwa sababu ya vumbi. Karoti inarutubisha seli za mwili na kuufanya usizeeke haraka. Hii inatokana na uwepo wa Vitamin A ambayo ni muhimu katika kuimarisha uwezo wa macho kuona.

Huifanya ngozi iwe nzuri na yenye afya. Iwapo utatumia kurutubisha ngozi yako, ikwangue karoti kwa kutumia grater kiasi unachotaka. Tia asali kijiko kimoja kikubwa (cha kulia chakula) mafuta ya nzai au Olive kijiko kimoja kikubwa na limau kijiko kimoja kikubwa. Changanya vizuri, kisha itumie kusugua mwilini sehemu yoyote unayotaka. Ukimaliza, subiri kwa hadi dakika 15 na zaidi kisha oga. Itasaidia kuondoa taka katika vinyweleo, kuifanya ngozi iwe laini na kuondoa mikunjo ya ngozi. Kumbuka inatakiwa asali mbichi na si asali yoyote.

Karoti husaidia kuondoa sumu na taka mwilini. Inaondoa mafuta yasiyotakiwa katika ini (cholesterol) na kuliwezesha lifanye kazi vizuri. Husafisha njia ya haja kubwa na husaidia kupata choo vizuri kwa kuzuia kuvimbiwa (constipation).

Karoti zinasaidia kufanya fizi na meno kuwa imara na kuchochea uzalishwaji wa mate. Pia inasaidia kuzuia ugonjwa wa kiharusi (stroke). Baadhi ya watafiti kutoka vyuo vikuu maarufu duniani wanasema ulaji wa karoti sita kwa wiki husaidia kuepuka kiharusi.

Pia wamegundua kwamba karoti zinatibu tatizo la kupoteza kumbukumbu miongoni mwa wazee. Karoti hupunguza hatari ya kupata shinikizo la damu kwani ulaji wa karoti husaidia mwili kupata madini muhimu ya Potassium ambayo husaidia kutanua mirija ya damu na kufanya damu kufika katika maeneo husika ya mwili kwa urahisi.

Zaidi ya kuongeza kinga mwilini, karoti pia husasidia kuzuia magonjwa mengine kama vile kisukari (diabetes), kansa pamoja na magonjwa ya moyo. Karoti huwa na Vitamin C ambayo ni muhimu sana kwa kusisimua seli nyeupe za damu (white blood cells).

You can share this post!

Pigo jingine kwa Aukot bunge la kaunti ya Lamu kuupiga teke...

SHANGAZI AKUJIBU: Natamani mume ila naogopa sana kuolewa...

adminleo