• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Kiburi cha Matiang’i, Boinnet na Kihalangwa kimeiletea Kenya aibu kuu – Jaji Odunga

Kiburi cha Matiang’i, Boinnet na Kihalangwa kimeiletea Kenya aibu kuu – Jaji Odunga

Na RICHARD MUNGUTI

KINYUME  na matarajio ya kila mmoja Jaji George Odunga Alhamisi alikataa kuwatimua kazini Waziri Fred Matiang’I , Inspekta Jenerali wa Polisi Joseph Boinnet na Mkurugenzi wa Idara ya Uhamiaji Meja Mstaafu Gordon Kihalangwa na badala yake kuagiza walipe faini ya Sh200,000.

Lakini watatu hawa hawapasi kufurahi kwani Jaji Odunga alisema yeyote atakaye kufuatilia suala hilo yuko huru kwani watatu hao wamekaidi vifungu nambari 10 na 6 vya Katiba vinavyowataka watumishi katika nyadhifa za umma waletee sifa na heshima taifa kwa kutii na kutekeleza sheria na maagizo ya mahakama.

“Matiang’i, Kihalangwa na Boinnet wameiletea nchi hii fedheha na aibu kwa kumsafirisha wakili Dkt Miguna Miguna kinyume cha maagizo ya hii mahakama akubaliwe kuingia nchini pasi masharti yoyote,” alisema Jaji Odunga.

Alisema idara ya uhamiaji ilikaidi agizo imkabidhi Dkt Miguna pasi ya kusafiria chini ya  uangalizi wa tume ya kitaifa ya kutetea haki za binadamu.

Jaji huyo alisema maafisa hao wakuu serikalini badala ya kutekeleza maagizo ya korti walimfurusha  Dkt Miguna baada ya kumdunga dawa akapoteza fahamu kisha wakamwingiza kwa ndege na kumsafirisha hadi Dubai.

Jaji Odunga alisema watatu hao walikaidi maagizo ya korti kwa madharau na kiburi kikuu.

Jaji alikataa kuamuru washikwe watumikie kifungo cha miaka mitatu kila mmoja akisema , “Ikiwa watatu hawa walionyesha kiburi kikuu jinsi hii na kukataa sio mara moja bali mara nne kutii maagizo ya korti , ni afisa mgani anayehudumu chini yao atathubutu kuwakamata na kuwasukuma jela kuanza kutumikia kifungo.

Hakuna. Hivyo hii mahakama haiwezi kutoa maagizo ambayo hayatatekelezwa. Sasa kila mmoja atalipa faini kutoka kwa mshahara wake ya Sh200,000.”

Agizo hilo litapelekwa kwa afisi ya rais na naibu wa msajili wa mahakama kuu. Pesa hizo zitawasilishwa kortini.

You can share this post!

Kambi za polisi zajengwa katika maeneo yanayolengwa na...

Wakili Mutinda aponea kusukumwa jela kwa kuwa...

adminleo