• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 6:27 PM
JAMVI: Muafaka ulivyoyeyusha siasa kali za Raila na NASA

JAMVI: Muafaka ulivyoyeyusha siasa kali za Raila na NASA

Na BENSON MATHEKA

HUENDA kinara wa NASA, Raila Odinga aliangukia mtego wa kuzima siasa zake kali za kuikosoa serikali kwa kukubali kushirikiana na Rais Uhuru Kenyatta.

Wadadisi wasema muafaka huo umemdhoofisha Raila kisiasa huku akikosa makali ya kukosoa serikali hata inapokiuka haki za washirika na wafuasi wake wa kisiasa.

Kulingana na wachanganuzi, huku dalili zikionyesha Raila alijikwaa kisiasa, Rais Kenyatta ameibuka mshindi baada ya  kiongozi huyo wa chama cha ODM kumtambua kama rais halali wa Kenya.

Wadadisi wanasema kufuatia muafaka huo, Raila alimtambua Uhuru Kenyatta kama Rais wa Kenya.

“Hilo ndilo lengo kuu la waliopanga mikakati ya muafaka huo na limeafikiwa,” alisema mdadisi wa masuala ya kisiasa, John Ondari.

Anasema jaribio la kurejea Kenya la wakili Miguna Miguna lilikuwa mtihani wa kwanza wa muafaka kati ya Raila na Rais Kenyatta lakini matukio yaliyofuatia tangu Jumatatu yameonyesha hali halisi ya muafaka huo.

“Kwamba Raila hakuweza kumshawishi Rais Kenyatta kuagiza maafisa wa serikali yake kumruhusu Miguna Miguna kuingia nchini ni dhihirisho kwamba muafaka huo ni hafifu,” alisema.

Kabla ya Bw Miguna kurejea nchini, ilisemekana moja ya makubaliano ya Raila na Rais Kenyatta ilikuwa ni kumruhusu wakili huyo kurudi Kenya.

Wakili James Orengo ambaye ni mshauri wa Bw Odinga alinukuliwa akisema, muafaka huo ungemwezesha Miguna kurudi nchi yake ya kuzaliwa bila kizingiti. Hata hivyo, licha ya kuwa na agizo la mahakama la kumruhusu kuingia nchini, Bw Miguna alizuiwa katika uwanja wa kimataifa wa ndege wa Jomo Kenyatta (JKIA).

Japo Raila alifika katika uwanja huo ambako Bw Miguna alizuiwa alipowasili Kenya Jumatatu mchana, hakuweza kumsaidia wakili huyo aliyemuapisha.

“Kilichotendeka ni maafisa wa polisi kumnyakua Bw Miguna mbele yake na kumsukuma kwa ndege wakiwa na maagizo ya kumfurusha nchini. Raila hakuweza kutumia ushirika wake mpya na Rais Kenyatta kumuokoa. Iwapo kurejea kwa Miguna kulikuwa moja ya makubaliano yao, basi alichezwa shere,” alisema.

Aliongeza kwamba, hata baada ya haki za wanahabari kukiukwa walipopigwa na maafisa wa usalama wakifuatilia kuzuiliwa kwa Miguna na masaibu aliyopitia, Raila hakutoa taarifa ilivyokuwa kawaida yake kabla ya muafaka wake na Rais Kenyatta.

Wadadisi wanasema Raila amejimaliza hivi kwamba ananyamaza serikali ikiendeleza ukatili aliokuwa akipinga kabla ya kukubali kushirikiana na Rais Kenyatta ikiwa ni pamoja na kukiuka maagizo ya mahakama.

“Alikuwa msitari wa mbele kutetea uhuru wa mahakama na ni miongoni mwa masuala ambayo alisema alikubaliana na Rais Kenyatta kuhakikisha yamezingatiwa.

Alikuwa msitari wa mbele kutaka mageuzi katika kikosi cha polisi ambao walimpuuza na kumkamata Bw Miguna mbele yake, alikuwa msitari wa mbele kutetea uhuru wa wanahabari ambao walipigwa wakifuatilia masaibu ya Bw Miguna na hajasema lolote,” alieleza.

 

Mateka wa Uhuru

Wachanganuzi wasema muafaka huo umemfanya mateka wa Rais Uhuru kiasi cha kunyamaza hata wakati serikali inawanyanyasa wafuasi wake.

“Ni kama anashindwa atakavyowaambia wafuasi wake baada  ya kugundua alifanya makosa. Baadhi yetu tunasikitika,” asema mbunge mmoja wa ODM ambaye aliomba tusitaje jina lake.

Mbali na masaibu ya Bw Miguna, amekuwa kimya hata mawakili wa ODM, miongoni mwao wabunge Otiende Amollo na James Orengo walipofurushwa JKIA.

“Muafaka huo umemfanya Raila kuwa mateka wa serikali. Kimya chake kinaonyesha alijifunga katika makubaliano yake na Rais Kenyatta. Serikali inaendelea kupuuza maagizo ya mahakama bila kujali akitazama tu. Tunashangaa ni nini alichopewa kukubali mkataba huo,” aeleza mbunge huyo.

Baada ya kutimuliwa JKIA Jumatano usiku, Bw Orengo alisema inaonyesha muafaka kati ya Raila na Uhuru hauna maana na umuhimu wowote. Raila mwenyewe hakushutumu kitendo hicho.

Baadhi ya wadadisi wanahisi Raila alichezewa shere kukubali kushirikiana na serikali ili kuzima nguvu za upinzani za kushinikiza mageuzi katika uchaguzi, uhuru wa mahakama, na mageuzi katika kikosi cha polisi miongoni mwa masuala mengine.

Wanasema Rais Kenyatta alitaka kuhudumu katika kipindi chake cha pili bila kuhangaishwa na ni Raila pekee anayeweza kumkosesha usingizi.

Siku chache baada ya kutangaza muafaka wao, kamati andalizi ya NASA kuhusu Bunge la Wananchi ilisitisha shughuli zake kutoa nafasi ya maridhiano na waliopanga muafaka huo wakawa wamepiga hatua muhimu.

 

Kutiwa mfukoni

“Jinsi muafaka huo ulivyochezwa ilikuwa mbinu ya kumvuta Raila karibu na kumweka mfukoni. Ulifanywa kwa siri ili kumtenga na vinara wenza wa NASA ambao tayari wamemshtumu na chama chake cha ODM kwa kuwasiliti.

Kwa kumvika nembo ya usaliti, upinzani ulizimwa  na kufuatia matukio ya hivi majuzi katika seneti, ni mlima kurejesha umoja wa NASA,” anaeleza Bw Tom Maosa wakili na mdadisi wa siasa ambaye kwa sasa yuko Sierra Leone.

Baada ya kutangaza muafaka wake na Rais Kenyatta, Raila aliongoza mkutano wa Wabunge wa chama chake cha ODM na wakakubali  kuunga mkono ushirikiano huo licha ya vinara wa vyama tanzu vya NASA Wiper, Ford Kenya na Amani National Congress (ANC) kulalamika jinsi mazungumzo yalivyofanyika kwa siri.

ODM kilimpokonya Moses Wetangula wadhifa wa Kiongozi wa Wachache katika seneti licha ya kuwa kinara mwenza wa NASA, jambo ambalo wadadisi wanasema lilikuwa msumari wa mwisho katika jeneza la NASA.

“Kuvunjika kwa NASA wakati Wetangula na Mudavadi (kiongozi wa ANC) walipotangaza kujipanga upya kisiasa kulikamilisha mchezo ambao waliopanga muafaka huo kumfunga  Raila walilenga,” asema.

Kufikia sasa, muafaka wao haujafafanuliwa kwa kina, japo Raila amekuwa akisisitiza kuwa hajajitenga na NASA licha ya chama chake cha ODM kutenga vyama tanzu.,

You can share this post!

TAHARIRI: Ukatili wa polisi dhidi ya waandishi ulikiuka haki

JAMVI: Huenda ushirikiano mpya wa Raila na Uhuru ukamfaa...

adminleo