• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
SENSA: Mbona serikali inatudharau?, Tharaka-Nithi yawaka

SENSA: Mbona serikali inatudharau?, Tharaka-Nithi yawaka

NA CECIL ODONGO

VIONGOZI kutoka kaunti ya Tharaka-Nithi wameapa kwenda mahakamani baada ya miezi sita ili kupinga matokeo ya idadi ya watu yaliyotolewa Jumatatu na kuonyesha kuwa kaunti hiyo ina watu 393,177.

Wakihutubia wanahabari jijini Nairobi Jumanne, Gavana wa kaunti hiyo Bw Muthomi Njuki, mbunge wa Tharaka, Bw Gitonga Murugara, mwenzake wa Chuka-Igambang’ombe Bw Patrick Munene na  yule wa Maara Bw Kareke Mbiuki walitishia kwenda mahakamani ili zoezi la kuhesabiwa kwa watu eneo hilo lirudiwe.

Walisema kaunti hiyo inaonewa kutokana na siasa za jopokazi la maridhiano (BBI) ilhali kura zake ziliokoa utawala wa Rais mstaafu Mwai Kibaki mwaka wa 2007.

“Tunakataa takwimu hizi kwa kuwa zinatumiwa kutimiza malengo ya kisiasa hapo 2022. Haiwezekani kamwe idadi ya watu wazima iwe kubwa kuliko ya watoto. Tutaelekea mahakamani iwapo KNBS haitarudia sensa eneo letu,” akafoka Gavana Njuki.

Kutoka kushoto: Mbunge wa Tharaka Bw Gitonga Murugara, Gavana wa kaunti hiyo Bw Muthomi Njuki, mbunge wa Maara Bw Kareke Mbiuki mwenzake wa Chuka-Igambang’ombe Bw Patrick Munene walipohutubia wanahabari jijini Nairobi, Jumanne. Picha/ Cecil Odongo

Bw Njuki aliongeza kuwa kulingana na matokeo ya idadi ya mwaka 2009, kaunti hiyo ilikuwa na watu 365,330 hivyo basi ni makosa kusema kuwa kwa muda wa miaka 10 ni watu 27, 847 ambao wameongezeka.

Alisema hilo ni kinyume na matarajio yao kuwa dalili zote zilionyesha kuwa idadi hiyo itakuwa imefika 480,000.

Kwa upande wake, Bw Mbiuki aliishangaa serikali kudharau eneo hilo kwa kukosa kutoa hesabu kamili ya watu kama maeneo mengine.

“Hazina Kuu inafaa kutoa fedha za kugharamia zoezi lingine la sensa kwa kuwa kaunti hii inatapata mgao wa chini na pia kubaguliwa katika utoaji wa ajira serikalini,” akasema.

Bw Munene naye alisema eneobunge lake limo hatarini kuvunjwa kwa kuwa kulingana na sheria inayopendekezwa, halifikishi watu 130,000.

Bw Murugara alitaja takwimu hizo kuwa feki na kuikejeli KNBS maanake wanaishi maisha sawa na wenzao wa Meru na Embu ambao idadi yao imeongezeka pakubwa.

You can share this post!

Kadhaa wanusurika kifo katika ajali Thika Superhighway

SENSA: Kila Mkenya anadaiwa Sh124,000

adminleo