• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:05 AM
SENSA: Kila Mkenya anadaiwa Sh124,000

SENSA: Kila Mkenya anadaiwa Sh124,000

Na LEONARD ONYANGO

MATOKEO ya Sensa yaliyotangazwa Jumatatu yamethibitisha kuwa kila Mkenya anadaiwa kiasi cha Sh124,000 ili kulipa jumla ya Sh5.9 trilioni ambazo Kenya inadaiwa.

Kulingana na matokeo hayo yaliyotangazwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Takwimu nchini (KNBS), Bw Zachary Mwangi, katika Ikulu ya Nairobi, Kenya ina jumla ya watu 47,564,296.

Kati yao wanawake ni 24,147,016 na wanaume 23,548,056 huku watu walio na jinsia mbili wakiwa 1,524.

Ripoti ya Hazina Kuu iliyowasilishwa katika Bunge la Kitaifa mwezi uliopita ilionyesha kuwa deni ambalo Kenya inadaiwa na wakopeshaji wa humu nchini na mataifa ya kigeni kama vile China, limefikia Sh5.902 trilioni.

Deni hilo likigawanywa kila Mkenya atatakiwa kulipa Sh124,084.

Matokeo ya Sensa pia yanaonyesha kuwa Wakenya wameongezeka kutoka milioni 37.7 hadi milioni 47.6 kati ya 2009 na 2019.

Hiyo inamaanisha kwamba Wakenya milioni 9.9 wameongezeka ndani ya kipindi cha miaka 10 iliyopita.

Hiyo inamaanisha kwamba watoto 2,710 huzaliwa humu nchini kwa siku. Hiyo ni sawa na watoto 225 kwa saa na watoto watatu kwa kila dakika.

Itahitajika viwanja 793 vyenye uwezo wa kubeba watu 60,000 kama vile Uwanja wa Kasarani ili kila Mkenya kupata nafasi.

Matokeo hayo ya sensa pia yamefichua kuwa takribani Wakenya milioni tisa hawakujisajili na Huduma Namba.

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia (ICT), Bw Joe Mucheru, mnamo Mei alisema kuwa Wakenya milioni 38 walijisajili na Huduma Namba.

Kulingana na matokeo ya sensa, kaunti 18 zina watu milioni moja na zaidi.

Kaunti ya Nairobi inaongoza kwa kuwa na idadi kubwa zaidi ya watu milioni 4.4 ikifuatiwa na Kiambu watu milioni 2.4 milioni.

Kaunti nyingine zilizo na zaidi ya watu milioni moja ni Nakuru (milioni 2.2 milioni), Kakamega (milioni 1.8), Bungoma (milioni 1.6), Meru (milioni 1.54), Kilifi (milioni 1.45), Machakos (milioni 1.4), Kisii (milioni 1.26) na Mombasa (milioni 1.2).

Nyingine ni Uasin Gishu (milioni 1.16), Narok (milioni 1.15), Kisumu (milioni 1.15), Kitui (milioni 1.13), Homa Bay (milioni 1.13), Kajiado (milioni 1.1) , Migori (milioni 1.1), Murang’a (milioni 1.05).

Kaunti sita zilizo na watu chini ya 400,000 ni Tharaka-Nithi , Taita/Taveta , Tana River, Samburu, Isiolo na Lamu.

“Wastani wa watu wanaoishi katika nyumba moja imepungua kutoka watu 4.2 mnamo 2009 hadi watu 3.9 mwaka huu,” akasema Bw Mwangi.

“Hiyo ni ripoti ya kwanza na shirika la KNBS litatoa ripoti nyingine zitakazoto ufafanuzi wa kina kuhusu idadi ya watu kuanzia katika ngazi ya lokesheni, shughuli za kiuchumi kati ya taarifa nyinginezo,” akaongezea.

Sensa hiyo iliyofanyika usiku wa Agosti 24 na Agosti 25, mwaka huu, ndiyo ya kwanza kufanyika chini ya Katiba ya 2010.

Akizungumza baada ya kukabidhiwa ripoti hiyo ya sensa, Rais Uhuru Kenyatta aliagiza wizara na mashirika ya umma kuzingatia takwimu za KNBS katika mipango ya miradi ya maendeleo.

“Ninaagiza wizara na mashirika yote ya serikali na hata serikali za kaunti kutumia takwimu zilizotolewa na KNBS katika mipango yote ya maendeleo,” akasema Rais Kenyatta.

You can share this post!

SENSA: Mbona serikali inatudharau?, Tharaka-Nithi yawaka

Aibu ya mashirika kulipa walinzi Sh4,000

adminleo