• Nairobi
  • Last Updated March 18th, 2024 8:55 PM
EACC yatofautiana na polisi kuhusu ufyatulianaji risasi na hongo

EACC yatofautiana na polisi kuhusu ufyatulianaji risasi na hongo

NA JUSTUS OCHIENG’

TUME ya Maadili ya Kupambana na Ufisadi(EACC) na polisi wametofautiana vikali kuhusu kisa cha kupigwa risasi wa maafisa wa tume hiyo waliokuwa wakiendesha operesheni ya kuwanyaka maafisa wa trafiki kuhusu hongo mjini Kisumu.

Maafisa hao wa tume hiyo walikuwa wamevamia mzunguko wa Mamboleo kwenye barabara ya Kisumu-Kakamega ambapo polisi walikuwa wakitekeleza wajibu wao.

Juhudi za maafisa wa EACC za kuwanyaka polisi waliodaiwa walikuwa wakipokea hongo ziliishia ufyatulianaji wa risasi huku polisi wawili wakinyakwa wakati wa kisa hicho.

Maafisa wa EACC pia walikuwa wameandaa operesheni kama hiyo katika kituo cha kibiashara cha Riat karibu na uwanja wa ndege wa Kisumu.

Kwenye kisa cha Mamboleo, afisa wa polisi wa trafiki kwa jina Gladys Chemutai alisalia na majeraha ya risasi kwenye mguu wake wa kulia huku mwenzake Fredrick Matunda pia akisalia na majeraha kwenye goti lake.

Afisa mwngine kwa jina Marwa Mwita naye alikamatwa. Kando na maafisa hao, polisi wengine wa trafiki waliokamatwa ni Meshack Munyendo, Wesley Koech na Benjamin Tuwei. Watano hao bado hawajafikishwa mahakamani, wiki moja baada ya kukamatwa.

Kulingana na Mkuu wa EACC ukanda wa Nyanza Aura Chibole, Bi Chemutai hakuwa kati ya walionyakwa na anaendelea kupokea matibabu katika hospitali ya Avenue baada ya kufanyiwa upasuaji mguuni.

Bw Matunda pia yupo kwenye hospitali hiyo akiganguliwa. EACC tayari imewaondolea lawama maafisa wake kuhusiana na tukio hilo na kuwashutumu polisi wa trafiki kwa kuwapiga risasi maafisa wenzao.

Bw Chibole wikendi alikuwa na wakati mgumu kueleza namna kisa hicho kilivyotokea, akisema tu kwamba bunduki zote za maafisa waliohusika zimetwaliwa ili kufanyiwa uchunguzi wa kitaalamu kujua ni ipi iliyotoa risasi iliyomdhuru Bi Chemutai.

“Maafisa wetu hawakufyatua risasi. Hayo ni madai ya polisi wa trafiki japo bunduki zote zilizotumika zimetwaliwa kufanyiwa uchunguzi wa kitaalam,” akasema Bw Chibole.

Kulingana na ripoti ya tukio hilo katika kituo cha polisi cha Kondele iliyoonekana na Taifa Leo, maafisa wa EACC wamehusishwa na ufyatulianaji wa risasi kama njia ya kuwaadhibu polisi wa trafiki wakati wa kukamatwa kwao.

Ripoti hiyo ya OCS wa Kondele James Nderitu iliyoandikwa kwa makao makuu ya polisi inasema kwamba maafisa wa EACC ndio walifyatua risasi kama njia ya kuwatia maafisa hao uoga ndipo wawakamate.

Taifa Leo imebaini kwamba Idara ya Uchunguzi wa Uhalifu(DCI) imeanzisha uchunguzi kuhusu tukio hilo huku Bw Chibole akiomba muda zaidi wa kumalizwa uchunguzi kwenye bunduki zilizotwaliwa.

Baadhi ya mashahidi tayari wameandikisha taarifa na DCI , taarifa zinazodaiwa kulaumu EACC kutokana na kosa hilo.

Maswali pia yameibuliwa kuhusu kucheleweshwa kwa mchakato wa kuwafikisha mahakamani maafisa watano wa polisi siku tano baada ya kisa hicho huku ikisemekana EACC bado haijaamua itawashtaki kwa kosa lipi.

Hata hivyo, Mkuu wa Polisi eneo la Nyanza Dkt Vincent Makokha alisema watashtakiwa mahakamani baada ya afisi ya Mkuu wa Mashtaka ya Umma kuipa EACC ruhusa.

You can share this post!

Genge linavyohangaisha wanawake na wasichana

Afa kwa kujirusha baharini toka ferini

adminleo