• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Kieleweke sasa wataka Kiunjuri avuliwe uwaziri

Kieleweke sasa wataka Kiunjuri avuliwe uwaziri

Na NDUNGU GACHANE

VIONGOZI wa kundi la Kieleweke wamemtaka Waziri wa Kilimo Mwangi Kiunjuri ajiuzulu wadhifa wake kisha ajiunge na Tangatanga baada ya kuhudhuria mkutano wa mrengo huo wiki jana mjini Embu.

Mbunge wa Nyeri Mjini Ngunjiri Wambugu amesema Bw Kiunjuri ameonyesha kwamba hatilii maanani majukumu yake ya uwaziri na sasa macho yake yanalenga siasa za 2022.

Bw Kiunjuri na zaidi ya viongozi 50 walikutana katika hoteli moja mjini Embu wiki jana na kuapa kushinikiza kuboreshwa kwa sekta ya kilimo cha majani chai, kahawa, nyanya na viazi katika ukanda wa Mlima Kenya.

Aidha, Bw Wambugu alishangaa kwa nini waziri huyo alikuwa akijumuika na wabunge hao ilhali wizara yake ndiyo ina majukumu ya kuhakikisha kuna mageuzi makubwa kwenye sekta ya kilimo aliyorejelea.

“Wakati wa mkutano huo nilimwoma Kimani Ichungwa (Kikuyu) ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya bajeti bungeni, Moses Kuria (Gatundu Kusini), mwanachama wa kamati hiyo pamoja na Bw Kiunjiri ambaye anafaa kutatua masuala hayo kama waziri, akilalamikia kudorora kwa sekta zetu za kilimo badala ya kuyatatua,” akasema Bw Wambugu.

Mbunge huyo ambaye anaegemea mrengo wa Kieleweke katika mvutano ndani ya Jubilee, anataka waziri Kiunjuri aondoke afisini mara moja.

“Ameshindwa kutekeleza majukumu aliyopewa na sasa anafanya kampeni za afisi ya kisiasa anayolenga kuwania mwaka wa 2022,” akasema Bw Wambugu.

Mbunge huyo alishikilia kwamba ni waziri huyo anayefaa kulaumiwa kwa kukosa kuangazia maslahi ya wakulima kutoka ukanda wote wa Mlima Kenya.

Bw Wambugu amekuwa mstari wa mbele kutetea ushirikiano kati ya Rais Uhuru Kenyatta na Kinara wa upinzani Raila Odinga.

Alidai kuwa viongozi wa Tangatanga wamekuwa wakijificha nyuma ya uungawaji mkono wa Naibu Rais William Ruto, ili kuwapumbaza wakazi wa Mlima Kenya.

“Nawaomba wakome kujificha nyuma ya uwaniaji wa Dkt Ruto 2022 kwa kutumia masaibu ya wakulima. Iwapo wanawajali basi hatungekuwa tukishuhudia malalamishi ya wakulima ikizingatiwa wanashikilia vyeo muhimu kwenye kamati za bunge na wizara,” akaongeza Bw Wambugu.

Kwa upande wake, mbunge wa Gatanga Nduati Ngugi alisema kwamba haikuwa vyema kwa Bw Kiunjuri kuhudhuria mkutano huo na kutoa wito kwa Rais Uhuru Kenyatta amfute kazi mara moja.

“Hatua lazima ichukuliwe dhidi ya Bw Kiunjuri kwa kuhudhuria mkutano ambao hauhusiani kivyovyote na utekelezaji wa sera za serikali. Rais Kenyatta ambaye ni kiongozi wa chama chetu pia amewaonya mawaziri wake mara kadhaa wakome kujihusisha na siasa,” akasema Bw Ngugi.

Aidha alisema mkutano huo wa Embu sasa umegawanya wakazi wa Mlima Kenya zaidi na akatoa wito kwa Naibu Rais awakomeshe viongozi wa Tangatanga ambao wamekuwa wakitoa matamshi makali dhidi ya mawaziri mbele yake.

“Chama chetu kinasimamia amani na umoja wa taifa hili na namrai Dkt Ruto awatulize wandani wake wenye tabia ya kupanda majukwaani na kuwatusi maafisa wa serikali ambao hawakubaliani nao kisiasa,” akaongeza Bw Ngugi.

You can share this post!

Sh500 milioni kwa atakayefichua aliko Jehad Serwan Mostafa

Yaibuka BBI sasa itachukua mkondo wa ‘Punguza...

adminleo