• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 4:31 PM
ODM yaionya Jubilee dhidi ya kuvuruga muafaka

ODM yaionya Jubilee dhidi ya kuvuruga muafaka

Na BARACK ODUOR

WABUNGE wa Chama cha ODM wameonya wenzao wa Jubilee dhidi ya kujaribu kuvuruga maelewano kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa upinzani, Bw Raila Odinga.

Mbunge Mwakilishi wa Kaunti ya Homa Bay, Bi Gladys Wanga, na Mbunge wa Dagoretti Kaskazini, Bw Simba Arati, wamedai kuna wabunge wa Jubilee ambao wanafanya njama kisiri kusambaratisha maelewano ya viongozi hao wawili.

Wakizungumza katika harambee ya kusaidia Kanisa la Gendia Seventh Day Adventist lililo katika Kaunti ya Homa Bay, viongozi hao walisema maelewano yaliyofanywa yamenuia kuleta umoja nchini.

Bi Wanga alimkashifu Kiongozi wa Wengi Bungeni, Bw Aden Duale, kwa kudai kuna wabunge wa ODM ambao wanapinga maelewano hayo.

“Ninataka kumwonya Bw Duale kuhusu matamshi aliyotoa hivi majuzi kwamba baadhi ya wabunge wa ODM hawaungi mkono maelewano. Hii ni kwa sababu sote tunaunga mkono hatua hiyo ambayo ndiyo pekee inayoweza kudumisha amani na utangamano nchini,” akasema.

Kwa upande wake, Bw Arati aliambia wabunge wa Jubilee wajitenge na matamshi ambayo yanaweza kusababisha mgawanyiko nchini.

Alisema matamshi aina hiyo yanaweza kufanya malengo ya maelewano hayo yasifanikishwe na hali hiyo itasababisha janga la kisiasa nchini.

“Kuna nia ya baadhi ya wenzetu katika Jubilee kuingilia makubaliano kati ya kiongozi wetu na kiongozi wao. Lakini haifai watudharau kwa sababu tunajua tulikotoka,” akasema Bw Arati.

Alitoa wito kuwe na heshima kati ya wabunge wa ODM na Jubilee ili kuendeleza mbele malengo ya makubaliano hayo.

“Kama wanataka kusambaratisha makubaliano hayo, pia sisi tunaweza kufanya hivyo kwa hivyo inafaa tuheshimiane,” akasema.

Bi Wanga pia alitumia nafasi hiyo kusambaza vyakula kwa zaidi ya familia 50 zilizoathirika na mafuriko katika wadi ya Karachuonyo Kaskazini, eneobunge la Karachuonyo.

Alisema maendeleo nchini yanaweza kupatikana tu kama kuna amani na utangamano nchini kote.

You can share this post!

Wataka bunge lipitishe sheria kulinda tiba za kiasili

Amri ya kubomoa jengo la gavana yakoroga seneta

adminleo