• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Mauti na vilio wakazi wakidai haki yao Kasarani

Mauti na vilio wakazi wakidai haki yao Kasarani

PETER MBURU na MARY WAMBUI

POLISI Alhamisi waliendelea kulaumiwa kwa kutumia nguvu kupita kiasi kukabiliana na waandamanaji waliokuwa wakilalamikia ubovu wa barabara ya Kasarani- Mwiki jijini Nairobi.

Wakazi hao jana walilaumu polisi kuwa Jumatano waliwapiga watu wawili risasi na mmoja alikufa. Madai tofauti yalisema kuwa watu wawili waliuawa na polisi siku hiyo.

Ripoti zilisema mvulana wa miaka 17, Stephen Machurusi alipigwa risasi kifuani na kuwa alifariki hospitalini.

“Tulimpata akiwa amelala ndipo tukamkimbiza hospitalini lakini tukaambiwa kuwa risasi ilipenyeza mahali hatari. Alikufa muda mfupi baadaye,” akasema Lilian Waringa, dadake marehemu.

Lakini polisi walisema wamethibitisha kifo cha mtu mmoja pekee na kusema bado hawajabaini kilichomuua.

“Kile tumethibitisha ni kuwa mtu mmoja alifariki na maafisa watano wa polisi wakajeruhiwa vibaya. Baada ya upasuaji wa maiti kufanyika ndipo tutajua kilichomuua,” OCPD wa Kasarani Peter Kimani akasema.

Wakati hayo yakijiri, viongozi, wakuu wa usalama Kasarani, maafisa wa Mamlaka ya Ujenzi wa barabara za miji (Kura), maafisa wa vyama vya wenye matatu eneo hilo na Kitengo cha Utekelezaji wa Miradi katika afisi ya Rais (PDU) waliafikiana kusitisha maandamano hayo yaliyoanza Jumatatu na kuanza urekebishaji wa barabara husika mara moja.

Katika mkutano huo ulioongozwa na Seneta wa Nairobi Johnson Sakaja, pande zote ziliafikiana kuwa ukarabati wa barabara ya Kasarani- Mwiki ungeanza mara moja na magari kurejelea kazi ya kusafirisha wakazi.

“Malalamishi ya wakazi wa Kasarani ni ya kweli na ni haki yao kwani hali ya barabara ni mbovu sana. Hata hivyo, matukio ambayo yamekuwa yakishuhudiwa siku hizo za maandamano hayakuwa ya kufurahiwa,” Bw Sakaja akasema.

Barabara hiyo ilikuwa imefanyiwa ukarabati 2018 lakini ikaharibika muda mfupi baadaye kutokana na ujenzi duni.

Hali katika barabara nyingi jijini Nairobi ni ya kusikitisha licha ya wakazi kulipa kodi za juu kila mara.

You can share this post!

Mwanamke motoni kwa kumuua mumewe mlevi

Kesi ya Sonko kuendelea

adminleo