• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:45 AM
AFYA: Yafahamu madhara ya unywaji pombe kupita kiasi

AFYA: Yafahamu madhara ya unywaji pombe kupita kiasi

Na MARGARET MAINA

[email protected]

WATU wengi wanapopumzika nyumbani au vilabuni, utawapata wakinywa pombe tofauti.

Lakini sio siri kuwa pombe husababisha matatizo makubwa ya kiafya, yakiwemo maradhi ya moyo, ini pamoja na majeraha yatokanayo na ajali zitokanazo na ulevi mathalani dereva kuendesha gari akiwa chakari.

Vinywaji vilivyotengenezwa kwa matunda bila kilevi ni bora zaidi kwa afya yako kuliko vile vyenye kilevi.

Matatizo ya moyo

Unywaji wa pombe kupindukia husababisha matatizo mbalimbali ya moyo. Mishipa ya moyo hudhoofika na kushindwa kusukuma damu. Hii inaweza kusababisha damu kuganda na kusababisha kiharusi.

Tatizo la ini

Unywaji wa pombe unaweza kusababisha maradhi ya ini. Uharibifu huu husababisha seli za ini kuwa makovu na kushindwa kufaya kazi vyema.

Shinikizo la damu

Unywaji wa pombe kupita kiasi kunaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa shinikizo la damu. Pombe inaweza kuathiri mfumo wa usukumaji wa damu mwilini; jambo ambalo husababisha shinikizo la damu na baadaye matatizo mengine kama kushindwa kwa figo, ini na kadhalika.

Ugonjwa wa anemia

Anemia ni ugonjwa unaotokana na kushindwa kwa seli nyekundu za damu kusafirisha oksijeni ya kutosha kwenda kwenye mwili. Hivyo, unywaji wa pombe hupunguza uwezo wa seli nyekundu za damu kusafirisha oksijeni ya kutosha hivyo kusababisha ugonjwa wa anemia.

Kusinyaa kwa ubongo

Mtu anapozeeka nao ubongo wake unazidi kusinyaa. Hivyo unywaji wa pombe huharakisha kusinyaa kwa ubongo. Hili husababisha matatizo yatokanayo na kusinyaa kwa ubongo kama vile kupoteza au kupungua kwa uwezo wa kumbukumbu.

Maumivu ya miguu (gout)

Gout ni ugonjwa wa miguu unaotokana na kukusanyika kwa asidi kwenye viungio vya mifupa. Mara nyingi ugonjwa huu hujitokeza sana majira ya baridi. Pombe imedhihirika kuchangia kwa kiasi kikubwa kutokea kwa ugonjwa huu.

Kusinyaa kwa uso na macho

Unywaji mkubwa wa pombe husababisha kusinyaa kwa uso na macho hasa kwa wale wanaokunywa usiku. Mara ngingi uwatazamapo wanywaji wakubwa wa pombe utaona hata sura zao zimebadilika na kuonekana zimezeeka au kuchoka kuliko awali.

You can share this post!

BBI: Viongozi zaidi ya 150 wa Jubilee wakutana Naivasha

MAPISHI NA UOKAJI: Mkate wa boflo

adminleo