• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Harambee Stars: Kutoka 105 hadi 113 FIFA

Harambee Stars: Kutoka 105 hadi 113 FIFA

Na GEOFFREY ANENE

HARAMBEE Stars ya Kenya imeporomoka nafasi nane kwenye viwango bora vya Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), Ijumaa.

Baada ya kulipuliwa 3-2 na Jamhuri ya Afrika ya Kati na kukabwa 1-1 na Comoro mwezi Machi, Kenya imetupwa kutoka nafasi ya 105 hadi 113.

Jamhuri ya Afrika ya Kati imepaa nafasi sita hadi nambari 115 nayo Comoro imeshuka nafasi tisa hadi 141.

Wapinzani wa Kenya katika mashindano ya kufuzu kushiriki Kombe la Afrika (AFCON) mwaka 2019, Ghana wamepaa nafasi tatu hadi nambari 51 duniani nao Sierra Leone na Ethiopia wakateremka kutoka 98 hadi 102 na 137 hadi 145, mtawalia.

Uganda inaongoza katika eneo la Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) katika nafasi ya 74 duniani baada ya kuimarika nafasi nne. Kenya ni ya pili katika Cecafa.

Inafuatwa na Rwanda (nafasi ya 123 duniani baada ya kushuka nafasi 13), Sudan (nafasi ya 126 duniani baada ya kuteremka nafasi tisa), Tanzania (imeruka juu nafasi tisa hadi 137 duniani), Ethiopia, Burundi (imeshuka nafasi tatau hadi 145 duniani), Sudan Kusini iko chini nafasi moja hadi nambari 155 nayo Djibouti inashikilia nafasi ya 198 baada ya kuporomoka nafasi 11.

Eritrea na Somalia zinavuta mkia katika nafasi ya 207 baada ya kushuka nafasi moja.

Tunisia inasalia nambari moja barani Afrika baada ya kupaa nafasi tisa hadi 14 duniani. Inafuatiwa na Senegal (chini nafasi moja hadi nambari 28 duniani), DR Congo (iko juu nafasi moja hadi 38 duniani), Morocco imesalia nafasi ya 42, Misri imeteremka nafasi mbili hadi nambari 46, Nigeria imeimarika nafasi tano hadi nambari 47 nayo Cameroon iko katika nafasi moja na Ghana baada ya kusalia nambari 51 duniani.

Kuna mabadiliko makubwa katika mduara wa timu 10-bora duniani. Ujerumani na Brazil zinasalia katika nafasi mbili za kwanza, mtawalia. Ubelgiji iko juu nafasi mbili hadi nambari tatu. reno na Argentina zimeshuka nafasi moja kila mmoja hadi nafasi za nne na tano nazo Uswizi na Ufaransa zimepaa nafasi mbili hadi nambari sita na saba, mtawalia.

Uhispania imeteremka nafasi mbili hadi nambari nane, Chile iko juu nafasi moja hadi nambari tisa nayo Poland, ambayo ililimwa 1-0 na Nigeria mnamo Machi 23, inafunga 10-bora baada ya kuteremka nafasi nne.

You can share this post!

Sekta za elimu na afya kufaidi pakubwa kwa bajeti ya ziada

Wakulima watoa sababu ya wanyakuzi kumezea mate ardhi zao

adminleo