• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 11:14 AM
Mhemuko Uhuru na Raila wakijipa raha mtindo wa Reggae

Mhemuko Uhuru na Raila wakijipa raha mtindo wa Reggae

Na LEONARD ONYANGO

RAIS Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM Raila Odinga walikuwa miongoni mwa mamia ya wapenzi wa muziki wa reggae waliojumuika katika ukumbi wa Carnivore jijini Nairobi kutumbuizwa na bendi kutoka Uingereza, Jumamosi usiku.

Kabla ya kwenda kuburudika, Rais Kenyatta Jumamosi alihudhuria hafla mbalimbali katika Kaunti za Meru na Kirinyaga huku Bw Odinga akiongoza mkutano wa kupigia debe ripoti ya Muafaka wa Maridhiano (BBI) katika Kaunti ya Kitui.

Video zilizosambazwa katika mitandao ya kijamii zinawaonyesha Rais Kenyatta na Bw Odinga wakionyesha weledi wao katika usakataji wa reggae ambao ni muziki unaohusishwa zaidi na jamii ya Rasta.

Rais Kenyatta husema wazi katika mahojiano jinsi anavyokienzi kikundi cha reggae cha UB40.

Miaka michache iliyopita, Bw Odinga pia aliambia kipindi cha Churchill Show ambacho hupeperushwa katika runinga ya NTV kila Jumapili jioni kwamba ni mpenzi wa muziki wa reggae.

“Wanamuziki wa reggae ninaowapenda zaidi ni kikundi cha UB40, Gregory Isaac na Bob Marley,” akasema Bw Odinga.

Katika mikutano ya BBI, Bw Odinga amekuwa akitumia wimbo wa Nobody Can Stop Reggae (hakuna mtu anayeweza kuzuia rege) wake Lucky Dube.

Bw Odinga amekuwa akitumia kibao hicho kwa maana kwamba hakuna mtu atakayezuia kura ya maamuzi ya kubadili katiba ili kujumuisha mapendekezo yaliyomo ndani ya ripoti ya BBI.

Kibao hicho chake Lucky Dube pia kilichezwa katika ukumbi wa Carnivore.

Katika moja ya video, Bw Odinga anaonekana jukwaani akisakata densi huku akipinda mgongo na kuchuchumaa.

Jana, Raila Odinga Junior, mwanawe Raila, alitia picha mtandaoni akimkabidhi kiongozi wa ODM mchongo wa picha ya Bob Marley.

“Nimemwonyesha Baba Raila Odinga mchongo huu wa Bob Marley aliopewa na ndugu yangu marehemu Fidel tuliporejea kutoka Kingston, Jamaica. Hakika hakuna mtu anayeweza kuzuia reggae,” akasema Raila Odinga.

Kwa upande mwingine, Rais Kenyatta aliyekuwa akisakata densi karibu na mwanahabari Jeff Koinange, anaonekana akiimba kwa kufuata mapigo ya muziki.

Kikosi cha UB40 kilichobuniwa mnamo 1978, kimejizolea umaarufu kutokana na nyimbo zake motomoto kama vile Red Red Wine. Kikundi hicho kiliundwa na ndugu wawili Ali Campbell na Robin Campbell kabla ya kukosana na kugawanyika mnamo 2008.

Waziri wa Michezo na Utamaduni Amina Mohamed alikaribisha bendi hiyo akisema uwepo wake nchini ni motisha kubwa kwa vijana wasanii.

You can share this post!

Wakazi walilia Gavana Kingi awape maji

Arsenal sasa majogoo wa kulazimisha sare

adminleo