• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 10:55 AM
Rais Mstaafu Moi anazidi kukumbukwa kwa mengi aliyotenda

Rais Mstaafu Moi anazidi kukumbukwa kwa mengi aliyotenda

Na LAWRENCE ONGARO

RAIS mstaafu Daniel Arap Moi atakumbukwa kwa kuridhia hatua muhimu ya mchakato wa urejeshwaji wa mfumo wa vyama vingi kwa nchi ya Kenya.

Mbunge wa Thika Bw Patrick ‘Jungle’ Wainaina, alituma salamu zake za pole alipozuru boma la Moi katika mtaa wa Kibera jijini Nairobi mnamo Jumatano.

Mbunge huyo alisema Moi anafaa kuheshimiwa sana kwa kuondoa kifungu cha 2A kilichoruhusu vyama vingi vya kisiasa kuingia nchini.

“Jambo hilo pekee ni muhimu kwa sababu atakumbukwa kwa miaka mingi kwa kuleta mabadiliko hayo licha ya wengi ‘kutabiri’ ya kwamba hilo halingetimia,” alisema Bw Wainaina.

Licha ya hayo alisema Bw Moi alifanya jambo la heshima na kung’atuka kutoka uongozini kwa heshima zake na kumkabidhi Bw Mwai Kibabi usukani mwaka wa 2002.

Aliongeza kuwa hata ingawa alisema kuwa atamkabidhi mwingine uongozi bado wengine walidai haingewezekana.

Jambo lingine la muhimu lililofanya akumbukwe na wengi ni kwamba shule za msingi zilipata fursa ya kunywa maziwa shuleni jambo lililosababisha watoto wengi kuhudhuria shule.

“Kutokana na mambo hayo matatu, Moi aliacha kielelezo ambacho kitakumbukwa na wengi katika kizazi kijacho,” alisema Bw Wainaina.

Bw James Karanja ambaye alikunywa maziwa ya ‘Nyayo’ anasema wanafunzi wengi walihudhuria shule bila kuchelewa kwa sababu ya kunywa maziwa shuleni.

“Mimi nakumbuka vyema ya kwamba wengi wetu tukiwa shule ya msingi hatukukosa kuhudhuria shule kwani tulijua ya kwamba tungekunywa maziwa shuleni. Hata familia maskini zilinufaika pakubwa na mradi huo wa kunywa maziwa shuleni,” alisema Bw Karanja.

Bw James Njuguna anakumbuka vyema wakimwimbia Moi njiani akielekea ziara za kukagua miradi ya maendeleo ambapo hakusahau kutoa fedha kidogo kwa wanafunzi wanywe soda.

“Nakumbuka vyema siku moja eneo la Nakuru tulimwimbia na baadaye akatoa pesa za soda kwa wanafunzi; jambo lililotufurahisha kabisa,” alisema Bw Njuguna.

Pia Moi alisifika kwa kufanya kazi kwa bidii bila kuchoka.

Imeelezwa alifanya mazoea kuingia Ikulu kabla ya saa moja za asubuhi na kuanza ziara zake za kukagua maendeleo mara moja.

Jambo lingine muhimu kwake ni kwamba alizuru karibu kila pembe ya nchi ya Kenya na kuelewa karibu kila kitu kilichotendeka nchini.

Wakuu wa mkoa hadi machifu walikuwa kiungo muhimu kwa utawala wa Moi ambapo waliweza kumjulisha karibu kila kitu kilichotendeka mashinani.

You can share this post!

Mahrez anyakua king’asti mwingine baada ya talaka

KIKOLEZO: EMB kama ‘ndrama’, kunani?

adminleo