• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:38 AM
Kirui kujizolea mamilioni kwa kusalia kileleni mwa jedwali

Kirui kujizolea mamilioni kwa kusalia kileleni mwa jedwali

Na GEOFFREY ANENE

LICHA ya kupoteza ubingwa wa mbio za Boston Marathon hapo Jumapili jioni, Mkenya Geoffrey Kirui anaongoza vita vya kujinyakulia tuzo ya Sh25 milioni kwenye Marathon Kuu Duniani (WMM) ya msimu wa 11.

Kirui, ambaye alijishindia Sh7.5 milioni kwa kumaliza makala ya 122 ya Boston Marathon katika nafasi ya pili, yuko juu ya jedwali kwa alama 41. Alipata alama 25 kwa kushinda Riadha za Dunia mnamo Agosti 6, 2017 na kujiongezea alama 16 kwa kumaliza wa pili nyuma ya Mjapani Yuki Kawauchi mjini Boston.

Bingwa wa Marathon Kuu Duniani wa msimu wa 11 atafahamika baada ya mbio za London Marathon nchini Uingereza hapo Aprili 22, 2018. Matumaini yake ya kushinda Marathon Kuu Duniani yatategemea sana matokeo ya Wakenya wenzake Daniel Wanjiru na Eliud Kipchoge.

Wanjiru yuko jijini London kutetea taji naye Kipchoge alishinda Berlin Marathon nchini Ujerumani mwaka 2017. Wawili hawa wamezoa alama 25. Mshindi hupata alama 25 kwa hivyo wawili hawa wanaweza kufikisha alama 50.

Bingwa wa Tokyo Marathon nchini Japan, Dickson Chumba na mshindi mpya wa Boston Marathon Kawauchi pia wana alama 25, lakini hawashiriki mbio za London. Makala ya 38 ya London Marathon hapo Aprili 22 yanatarajiwa kuwa moto kwa sababu yamevutia Wanjiru, Kipchoge na mahasimu wakubwa wa Kenya, Mo Farah (Uingereza) na Kenenisa Bekele (Ethiopia).

Vita vya taji la wanawake jijini London pia vinatarajiwa kuwa vikali. Mshikilizi wa rekodi ya dunia ya marathon ya wanawake pekee Mary Keitany (saa 2:17:01) atakabililiana na Muethiopia bingwa wa Chicago Marathon Tirunesh Dibaba (Ethiopia). Wawili hawa wanaongoza jedwali la wanawake la Marathon Kuu Duniani kwa alama 41 kila mmoja. Kipchoge anatafuta taji lake la tatu mfululizo la Marathon Kuu Duniani baada ya kushinda msimu wa tisa na 10.

Keitany pia ni bingwa mara mbili wa Marathon Kuu Duniani. Alishinda msimu wa sita na tisa.

Msimamo wa Marathon Kuu Duniani (5-bora):

Wanaume

Geoffrey Kirui (Kenya) alama 41

Dickson Chumba (Kenya) 25

Yuki Kawauchi (Japan) 25

Daniel Wanjiru (Kenya) 25

Eliud Kipchoge (Kenya) 25

Wanawake

Mary Keitany (Kenya) alama 41

Tirunesh Dibaba (Ethiopia) 41

Ruti Aga (Ethiopia) 32

Rose Chelimo (Bahrain) 25

Shalane Flanagan (Marekani)

Matokeo ya Boston Marathon (2018):

Wanaume

Yuki Kawauchi (Japan) saa 2:15:58

Geoffrey Kirui (Kenya) 2:18:23

Shadrack Biwott (Marekani) 2:18:35

Tyler Pennel (Marekani) 2:18:57

Andrew Bumbalough (Marekani) 2:19:52

Scott Smith (Marekani) 2:21:47

Abdi Nageeye (Uholanzi) 2:23:16

Elkanah Kibet (Marekani) 2:23:37

Reid Coolsaet (Canada) 2:25:02

Daniel Vassallo (Marekani) 2:27:50

Wanawake

Desiree Linden (Marekani) 2:39:54

Sarah Sellers (Marekani) 2:44:04

Krista Duchene (Canada) 2:44:20

Rachel Hyland (Marekani) 2:44:29

Jessica Chichester (Marekani) 2:45:23

Nicole Dimercurio (Marekani) 2:45:52

Shalane Flanagan (Marekani) 2:46:31

Kimi Reed (Marekani) 2:46:47

Edna Kiplagat (Kenya) 2:47:14

Hiroko Yoshitomi (Japan) 2:48:29

You can share this post!

Madiwani wapunjwa na ‘kamanda wa polisi’

Pigo kwa Gor Tuyisenge kukosa stakabadhi za kusafiri Afrika...

adminleo