• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
SENSA: Walemavu wengi ni wanawake

SENSA: Walemavu wengi ni wanawake

Na PETER MBURU

WANAWAKE wengi wako na ulemavu ikilinganishwa na wanaume, kulingana na ripoti ya sensa iliyofanywa 2019.

Ripoti hiyo inaonyesha kuwa kati ya watu 918, 270 wa zaidi ya miaka mitano waliorekodiwa kuwa na ulemavu wakati wa sensa Agosti mwaka jana, wanawake ni 523,883.

Wakazi wa mashambani pia walichangia idadi kubwa ya walemavu kwa visa 738,778, nao wa mijini wakijumuisha 179,492. Mashambani, wanawake 422,678 waliripoti kuwa na ulemavu, wanaume wakiwa 316,071.

Mijini nako kati ya walemavu 179,492, idadi ya wanawake ilikuwa juu, wakiwa 101,205.

Kaunti iliyoripoti visa vingi vya ulemavu Kenya ni Kakamega kwa visa 47,919, kati ya idadi hiyo wanawake wakiwa 27,546.

Kaunti ya Nairobi ilifuata kwa walemavu 42,703, ambapo wanawake walikuwa 23,322. Katika kaunti hiyo, eneo la Embakasi ndilo limeathirika zaidi kwa visa 7,137, likifuatwa na Kasarani kwa visa 6,719, nalo la Makadara likiwa na visa vichache zaidi, 1,955.

Kitaifa, eneo la Kibwezi katika Kaunti ya Makueni lilikuwa na walemavu wengi zaidi wakiwa 7,962, ambapo wanawake walijumuisha 4,693.

Aina za ulemavu zilizoripotiwa zaidi ni wa kutembea, kuona, kusikia, wa akili, uwezo wa kujitunza na mawasiliano.

Wakenya 385,417 wana ulemavu wa kutembea, 333,520 wana ulemavu wa macho, 212,798 wa akili, 153,361 ulemavu wa kusikia, wengine 139,929 shida za kujitunza na wasioweza kuzungumza vyema ni 111,356.

Katika Kaunti ya Nairobi, ulemavu ulioathiri watu wengi ni ule wa macho ambapo kuna watu 18,790 kisha wa kutembea kwa visa 14,551.

Katika aina zote za ulemavu, ni katika ule wa mawasiliano pekee ambapo idadi ya wanaume inazidi ya wanawake, zikiwa 60,701 na 50,641 mtawalia.

Idadi ya mazeruzeru (albino) pia ilirekodiwa kuwa 9,729, kati yao wanaume wakiwa 4,467 na wanawake 5,261. Kaunti ya Kakamega ilirekodi kuwa na idadi ya juu zaidi ya mazeruzeru wakiwa 568, ikifuatwa na ya Meru ambapo wako 563. Kaunti za Lamu na Isiolo zilikuwa na visa vichache zaidi, kwa mazeruzeru 17 na 20 mtawalia.

Jumla ya watu 7,652 hawakueleza ikiwa walikuwa ama hawakuwa na ulemavu, kati yao wanaume wakiwa 3,821 na wanawake 3,827.

You can share this post!

SENSA: Wakenya 20,000 hulala nje penye baridi kila siku

SENSA: Kina mama 180,000 hujifungulia nyumbani

adminleo