• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Tunahangaishwa kwa kupiga vita pombe haramu – Nyumba Kumi

Tunahangaishwa kwa kupiga vita pombe haramu – Nyumba Kumi

Na Phyllis Musasia

VIONGOZI wa Nyumba Kumi eneo la Kuresoi Kusini, wametishia kususia majukumu yao kwa madai ya kunyanyaswa na polisi.

Kupitia Michael Onyino wa Keringet mjini, walisema wamekuwa wakiteswa na hata kutishiwa maisha na polisi kila wanapotilia mkazo visa vya wakazi kujihusisha na biashara ya pombe haramu.

Wengi wao walidai kupigwa mbele ya washtakiwa na kutishiwa kukamatwa haswa wanapoonekana wakifuatilia na kusisitiza kuhusu baadhi ya kesi za jinai kwenye maeneo yao.

“Eneo hili limegeuka kuwa sehemu ambapo majangili wanaweza kutekeleza uhalifu wa aina yoyote ile na kisha waendelee kuishi maisha yao kama kawaida. Polisi wameonyesha kutoshughulika na yeyote hata unapowapa habari,” akasema Bw Onyino.

Aidha, baadhi ya wanafunzi wa shule za msingi wanatumika vibaya na majambazi kwa kununuliwa pombe na kisha kutumwa kuvunja nyumba za wakazi.

 

Kwenye kisa cha hivi maajuzi, Bw Onyino alidai kuwa kiongozi mmoja aliwakamata baadhi ya wanafunzi waliokuwa walevi na alipowapeleka katika kituo cha polisi cha Keringet, maafisa wa polisi waliokuwa kwenye zamu walimfukuza pamoja na wanafunzi hao na kudai kwamba kituo hicho hakina seli ya watoto.

“Alielezwa kuwa aondoke mara moja la sivyo akamatwe na kuwekwa ndani ya seli,” akaeleza Bw Onyino.

Kiongozi mwingine Bw Reuben Cheruiyot alisema mji wote wa Keringet uko gizani baada ya taa za usalama kuvunjwa na kuharibiwa na wezi usiku.

“Polisi wana habari hizi na hata machifu lakini muda umeyoyoma tangu kufanyika kwa kisa hiki bila yeyote kumatwa,” akasema.

Viongozi hao walisema wamedhalilishwa na kuonekana kama watu ambao hawafai kabisa katika jamii.

“Kazi yetu inatambulika na serikali lakini tunaifanya kama kazi ya kujitolea. Hakuna mshahara tunayopata lakini unapata kwamba tunadharauliwa kiasi cha haja,” akasema Bw Cheruiyot.

Walimkashifu naibu kamishna wa eneo hilo Patrick Mwangi kwa kukosa kuwahusisha katika mikutano ya maswala ya usalama.

Hata hivyo, Bw Mwangi alisema katika mahojiano kwamba hana habari kuwa viongozi wa Nyumba Kumi wanateswa na polisi. Aliwataka waandikishe malalamishi hayo katika ofisi yake.

Alisema anaheshimu viongozi wote wakubwa kwa wadogo kwa kazi wanayoifanya.

“Nimeandaa mkutano na machifu wa hapa utakaofanyika Jumanne wiki ijayo ili tujadiliane maswala haya. Kila kiongozi atahusishwa katika mipango wetu wa Keringet na hakuna atakayewachwa nje,” akasema.

Aliongeza kwamba yeye ni mgeni eneo hilo lakini ana matumaini kwamba malalamishi yote yatatatuliwa.

Aidha, kamanda wa polisi kaunti ya Nakuru Stephen Matu alisema hajapokea malalamishi hayo lakini yuko tayari kufuatilia na maafisa wa polisi wa eneo la Keringet ili kupata suluhu.

“Sina habari zozote kuhusu malalamishi haya lakini nitamtafuta naibu kamanda wa eneo bunge la Kuresoi Kusini kujua ni nini haswa kinachoendelea,” akasema Bw Matu.

You can share this post!

Mahakama yaamuru Wachina wanne warudishwe kwao

Coronavirus sasa yafika Afrika, Algeria yatangulia

adminleo