• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Wakazi wa Thika wapata maji kwa wingi

Wakazi wa Thika wapata maji kwa wingi

Na LAWRENCE ONGARO

WAKAZI wa Landless, Thika na maeneo ya karibu wamepata afueni baada ya kuletewa maji kwa wingi katika makazi yao.

Kikosi cha jeshi cha 12th Engineering Batalion, kwa mapatano na mbunge wa Thika Bw Patrick Wainaina kilifanikisha juhudi hiyo ya kupata maji.

Maji hayo yalichimbwa na kikosi hicho kwa siku mbili pekee kabla ya maji hayo kuonekana.

Bw Wainaina alisema alilazimika kuzungumza na kikosi cha jeshi kwa sababu wao wana uwezo wa kuchimba maji katika maeneo tofauti nchini.

“Ninapongeza juhudi za wanajeshi hao ambao walionyesha ujasiri wao kwa kufanya kazi hiyo mara moja bila kusita. Nimeridhika kwa sababu wakazi wa Thika sasa watanufaika na maji safi,” alisema Wainaina.

Alisema baadhi ya mitaa itakayonufaika pakubwa na maji hayo ni Landless, Gatundu, Muguga, na Ngoliba.

Alisema baada ya wakazi hao kupitia shida hiyo ya maji sasa atafanya juhudi kuona ya kwamba barabara za kisasa zinakarabatiwa ili waweze kuendesha biashara zao bila matata.

Afisa mkuu wa jeshi kikosi cha 12th Batalion Brigadier Geoffrey Radina, alisema maji hayo yatazidi kunywewa kwa muda mrefu na wakazi wa Thika.

“Sisi tayari tumefanya kazi yetu na sasa kilichobaki ni wananchi walinde mali yao ili wahalifu wasije wakaiba vifaa vilivyo hapo,” alisema Bw Radina.

Alisema kikosi chao cha Engineering Batalion kinafanya kazi kila sehemu nchini na kwa hivyo wameridhika na kazi hiyo waliyofanya.

Alieleza ya kwamba mradi huo umegharimu takribani Sh720 milioni, huku ukiwa ni wa kima cha urefu wa mita 130 ambapo ni fiti 400.

Mkurugenzi wa kampuni ya maji ya Thiwasco Water Company Ltd Bw Moses Kinya alisema kampuni hiyo itafanya juhudi kuona ya kwamba maji hayo yamefanyiwa ukaguzi maalum katika maabara ili kuhakikisha ni safi kwa binadamu.

Mbunge wa Thika Bw Patrick Wainaina ahutubu. Picha/ Lawrence Ongaro

Alisema watalazimika kuona ya kwamba wanaweka mabomba za kisasa za kusambaza maji katika mitaa tofauti.

“Tayari Benki ya Dunia imewasilisha Sh764 milioni kwa kampuni ya Thiwasco Water Company Ltd ili kujenga kituo cha kusambaza maji katika eneo la Mary Hill Mang’u,” alisema Bw Kinya.

Alisema kuongezeka kwa wakazi wa Thika kumewapatia changamoto kubwa na hivyo kutakikana kutafuta mbinu ya kuongeza maji kwa wingi.

Bi Stella Njeri ambaye ni mkazi wa mtaa wa Landless amefurahia kupata maji katika nyumba yake akisema shida ya zaidi ya miaka sita imekwisha.

“Kwa muda mrefu sasa sisi kama wakazi wa eneo hili tumepata shida kubwa ya maji lakini kwa huruma wa mbunge wetu sasa tuna maji,” alisema Bi Njeri na kuongeza “tutahakikisha tunalinda eneo hili lisije likavamiwa na wezi wa vifaa vya maji”.

You can share this post!

MASIKITIKO! Arsenal yachabangwa 2-1 na Olympiacos

MWANAMKE MWELEDI: Nembo ya uthabiti na ukakamavu katika...

adminleo