• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 9:50 AM
Wakenya wamkaanga Raila kwa kuwashauri wanawe mikono badala ya kuwapa msaada

Wakenya wamkaanga Raila kwa kuwashauri wanawe mikono badala ya kuwapa msaada

Na GEOFFREY ANENE

KIONGOZI wa Chama cha ODM Raila Odinga amejipata pabaya baada ya kuandikia Wakenya barua akiwakumbusha kuepuka mikusanyiko, wajitenge, wanawe mikono, wakae nyumbani na wavalie barakoa, hata za kujishonea ili kupiga jeki vita dhidi ya ugonjwa wa Covid-19.

Licha ya ujumbe unaonekana kuwa wa busara kutoka kwa afisi ya Bw Odinga mnamo Aprili 3, watumiaji wengi wa mitandao ya kijamii wamemkaanga waziri huyo wa zamani mkuu wakitaka aonyeshe ukarimu wake kwa kuchangia kwa hali na mali katika kuzuia maambukizi ya virusi vya corona vinavyosababisha ugonjwa huo ambao umeua watu wanne nchini Kenya na karibu 16, 000 kote duniani.

Baada ya barua hiyo kuchapishwa kwenye mtandao wa Twitter, Chebet alimwambia Bw Odinga, “Wewe andika barua nyingi unavyotaka, lakini nakueleza kuwa Wakenya hawatakula barua. Wanahitaji chakula na hiyo ndio njia ya pekee itakayowafanya wasitoke nyumbani. Ambia watoto wako mambo hayo mengine unatuambia.”

Liverpool 001 anasema, “Sijawahi kuona Raila akitoa mchango wake kusaidia wanaohitaji msaada. Hutawahi kumuona akifanya kile (Gavana) Joho, (Naibu Rais) Ruto ama (Gavana) Sonko hufanya. Sijui huwa anafanyia nini fedha zake zote?”

Kevin Omenya hakuwa na maneno mengi kwa Bw Odinga. Alisema, “Sijawahi kukuona ukitoa mchango wako.”

Nick K Ruto alishukuru Bw Odinga kwa ujumbe wake akisema, “Asante kwa kukumbusha Wakenya kuwa tuko katika hali mbaya. Hata hivyo, Mungu atatulinda.”

Naye OnePeopleOneTribeOneKenya alisema hana imani na wanasiasa. “Imani yangu kwa wanasiasa wa Kenya iliisha. Sasa ni wakati wa kuomba Mungu jinsi maandiko ya Isaiah 26:20 yanasema, “Endeni nyumbani, watu wangu, na mfunge milango yenu! Jificheni kwa muda hadi hasira ya Mungu itakapoisha.”

E K Gitau alijibu Bw Odinga akisema, “Ni lini utatoa sehemu ya mabilioni hayo yako kwa kusaidia katika vita hivi? Ama fedha zako umetengea shughuli ya kura ya maamuzi ya mwezi Juni?”

Ochiro alitaka kujua kiasi cha fedha Bw Odinga anachangia katika vita hivi. “Wewe unachangia fedha kiasi gani kusaidia watu walio katika hatari ya kuambukizwa virusi hivi na ambao hawana uwezo wa kununua chakula?”

mwania Simon alisema hajaona Bw Odinga akitoa msaada wa chakula kwa mwananchi wa kawaida ambaye anategemea kufanya kibarua kila siku kujikimu.

Sylvia Wangeci alisema barua ya Bw Odinga imejaa maneno mazuri, lakini “tunahitaji chakula ili kutushawishi tukae nyumbani.”

Justus Sila alitaka Bw Odinga atumie urafiki wake ndani na nje ya Kenya kuomba rafiki zake kutoa misaada ya chakula “hasa kwa wakazi wa mtaa wa Kibra kwa sababu tunajua huwezi hata kuchangia hata pakiti moja unga kwa mtu aliye katika hatari ya kufa njaa.”

Hilda Nabiswa alitaka Bw Odinga aonyoshe anachosema kwa vitendo. “Hatuna tatizo na barua yako. Sasa, hebu tuma magunia ya chakula mtaani Kibera. Hebu kuwa mstari wa mbele kwa kuonyesha kwa vitendo.”

You can share this post!

CORONA: Wanaosafiri kwa kaunti mpya kupimwa

Wakazi wa Korogocho wanufaika na mitungi ya maji na vieuzi

adminleo