• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 8:55 AM
Mvua kubwa yasababisha hasara Ruiru

Mvua kubwa yasababisha hasara Ruiru

Na LAWRENCE ONGARO

FAMILIA zaidi ya 200 katika vijiji vya Kimbo na Juja wameachwa na mahangaiko baada ya mvua kubwa kusababisha maji ya mafuriko kuingia katika nyumba zao.

Wakazi hao walisema usiku wa kuamkia Jumamosi walipata maji mengi ndani ya nyumba zao.

Kwa wakati huu wamebaki bila makazi maalum huku wakiomba serikali kuingilia kati ili kuwajali.

Mkazi wa Kimbo katika mji wa Ruiru, Kaunti ya Kiambu, Bi Jane Njeri alisema walirauka kuchota maji yaliyofurika katika nyumba zao.

“Nilirauka mwendo wa saa tisa za alfajiri na nikapata maji kwenye nyumba yangu. Sasa mali yangu yote imeloa maji huku nikishindwa jambo la kufanya,” alisema Bi Njeri.

Wakazi hao wanalaumu barabara kuu ya Thika Superhighway kwa sababu ndiyo inayosomba maji yote ya mvua hadi katika makazi yao.

“Wakati huu ndiyo viongozi wanastahili kujitokeza ili kusaidia wananchi walioathirika. Sasa tumeshindwa hata kuendesha biashara zetu. Tunaomba usaidizi wa dharura,” alisema.

Kwa muda wa wiki moja iliyopita mvua kubwa imenyesha kote nchini na kusababisha maafa mengi katika maeneo mengi.

Wakazi hao pia wanadai wezi wanaendelea kutekeleza wizi hata wakati huu mvua inaponyesha.

Mkazi wa Juja Bw James Mwangi alisema ilipofika usiku wa manane, kuamkia Jumamosi, alilazimika kukesha hadi asubuhi baada ya maji kufurika katika nyumba yake.

“Sisi wakazi wa hapa Juja tumepata hasara kubwa kabisa kwa sababu biashara nyingi zimekwama. Sasa tunaomba serikali kuingilia kati ili kutusaidia,” alisema Bw Mwangi.

Naye mkazi wa kijiji cha Kimbo, Ruiru Bi Jane Wangari alisema biashara nyingi zimekwama baada ya mafuriko hayo kushuhudiwa.

“Wakazi wa kijiji chetu wameathirika kabisa ambapo serikali inastahili kutusaidia ili tuendelee na shughuli zetu,” alisema Bi Wangari.

Alisema hata mifugo yao imeathirika ambapo wanakosa malisho maalum kufuatia mvua hiyo.

Idara ya Utabiri wa Hali ya Hewa imesema mnamo wikendi kwamba mvua nyingi inayoshuhudiwa kote nchini itaanza kupungua Mei 1, 2020.

You can share this post!

Saka kuwa kizibo cha Sancho kambini mwa Dortmund

Uhalifu umepungua kwa asilimia 50 – Kibicho

adminleo