• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 7:55 AM
COVID-19: Balala asema sekta ya utalii inapoteza Sh13bn kila mwezi

COVID-19: Balala asema sekta ya utalii inapoteza Sh13bn kila mwezi

Na WINNIE ATIENO

WAZIRI wa Utalii Najib Balala amesema sekta hiyo inapoteza takribani Sh13 bilioni kila mwezi kufuatia mlipuko wa virusi vya corona duniani.

Akiongea kwenye mahojiano na runinga moja nchini, waziri Balala amesema ugonjwa wa Covid-19 umesababisha sekta hiyo kudorora.

“Sekta hii ni muhimu sana katika uchumi wetu ikizingatiwa inaajiri watu 1.6 milioni lakini sasa kila mwezi tunapoteza Sh13 bilioni. Zaidi ya asilimia 90 ya sekta hii imefungwa na tunapoteza ajira na ushuru,” akasema waziri.

Hata hivyo, ameelezea matumaini yake kwamba sekta hiyo itaimarika.

Amesema wawekezaji wa sekta ya utalii wanafaa kukumbatia utalii wa nyumbani ili kufufua sekta hiyo badala ya kushughulikia wageni wa kimataifa.

Amewashajiisha kuhakikisha wanafanya utalii wa humu nchini wa gharama nafuu kwa Wakenya.

“Tunafaa kujua wageni wetu wanataka nini ili tupunguze bei ya utalii wa humu nchini. Pia tunataka wageni watembee sehemu zote nchini ingawa changamoto zilizopo ni miundombinu duni,” akasema Bw Balala.

Waziri amesema baada ya jinamizi la mlipuko huu sekta hiyo itaimarika huku akiwataka wawekezaji kujitayarisha kupata wageni.

Amewataka wawekezaji wa mikahawa na hoteli kufuata maagizo ya Wizara ya Afya ili kukabiliana na ugonjwa huo.

Amesema hatua ya serikali kufungua baadhi ya mikahawa itasaidia kukuza uchumi.

Amesema licha ya ugonjwa huo kuyumbisha sekta ya utalii, Wakenya wanaweza kukabiliana nao.

“Kama mikahawa hiyo itafuata maagizo basi tutaendelea kupata wageni zaidi baadaye. Osha mikono na sabuni, vaa barakoa na uhakikishe unazingatia kuwa mbali kwa angalau mita chache baina yako na mwenzako,” amesema waziri huyo.

You can share this post!

Serikali yasitisha ubomoaji zaidi Kariobangi

Soko la Tononoka hatari, mtaalamu wa afya aonya

adminleo