• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 9:55 AM
Kanisa la PCEA lawapa chakula wahitaji wa msaada

Kanisa la PCEA lawapa chakula wahitaji wa msaada

Na LAWRENCE ONGARO

KANISA la PCEA Makongeni, Thika, linaendelea kuwasaidia watu wa kipato cha chini kwa kuwapa chakula ikiwa ni njia mojawapo ya kukabiliana na janga la corona.

Kulingana na mpangilio wanufaika wanapokea chakula hicho Jumatano, Alhamisi na Ijumaa.

Mchungaji Rev, Simon Githiora Njuguna, ambaye ndiye msimamizi wa shughuli hiyo alisema hata watu wa imani tofauti za kidini wananufaika na mpango huo lakini ni sharti wawe na barua maalum kutoka wasimamizi wao katika maswala ya kidini kuelezea kuwa wako katika hali ngumu.

“Tulianzisha mpango huo mwanzoni mwa Machi na tutazidi kuwafaa kwa kuwakabidhi chakula,” akasema Bw Njoroge.

Alisema hadi sasa familia zaidi ya 500 kutoka maeneo tofauti zimefaidika pakubwa ambapo mpango huo umekuwa wa kufana zaidi.

Kulingana na Bw Njuguna, watu hao wanapokea kila mmoja mafuta ya kupikia lita moja, unga wa ugali kilo nne, maharage kilo mbili, mchele kilo mbili, na sabuni ya kipande mti mmoja.

“Baada ya kuzunguka maeneo tofauti tuligundua ya kwamba watu wengi hawana uwezo wowote wa kujilisha na kwa hivyo tulilazimika kama washirika kuungana pamoja kwa lengo la kusaidia wasiojiweza,” alisema Bw Njuguna.

Alisema jumla ya makanisa sita kutoka kaunti za Kiambu na Murang’a yaliamua kutoa msaada huo.

Baadhi ya makanisa hayo ni lile la Makongeni PCEA , Delmonte, Amani, Nanga (Murang’a), Mwana Wikio (Murang’a) na Thika PCEA Makongeni.

Baadhi ya wanufaika wa msaada uliotolewa na kanisa la PCEA mjini Thika. PIcha/ Lawrence Ongaro

Alisema mpango huo umekuwa ukiendeshwa kwa uwazi ambapo kila mmoja hupata haki yake bila utata wowote.

“Wakati huo pia sisi huwa mstari wa mbele kuwahamasisha kuhusu umuhimu wa kuzingatia usafi jinsi serikali inavyoagiza,” alisema Bw Njuguna.

Alisema jambo muhimu wanaoshauriwa kufuata ni kunawa mikono kila mara, kuvalia barakoa, kuweka zingatio la umbali wa mita moja au zaidi baina ya mtu na mwingine.

You can share this post!

Wito serikali iweke vifaa muhimu kwa ajili ya walemavu...

Harlequins yaanza kujisuka upya kwa msimu ujao wa raga ya...

adminleo