• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 6:55 AM
Serikali ya kaunti ya Mombasa yabuni mkakati wa kuipiga jeki sekta ya utalii

Serikali ya kaunti ya Mombasa yabuni mkakati wa kuipiga jeki sekta ya utalii

Na WINNIE ATIENO

WAWEKEZAJI wa sekta ya utalii wamepata afueni baada ya serikali ya Mombasa kutangaza mpango mpya wa kuwanusuru dhidi ya ada wanazotozwa kufuatia hali ngumu ya uchumi.

Aidha serikali hiyo inayoongozwa na Gavana Hassan Joho imesema itawanusuru wafanyabiashara wanaohudumu katika sekta ya utalii ambayo ndiyo inapitia changamoto kufuatia ukosefu wa watalii.

Sekta hiyo imeathirika kufuatia kusitishwa kwa safari za ndege za kimataifa katika nchi nyingi duniani ili kuzuia maambukizi ya homa ya corona.

Nchini Kenya hoteli nyingi za hadhi zimefungwa na wafanyakazi kusimamishwa kazi huku wengine wakilazimika kuchukua likizo.

“Serikali ya Kaunti ya Mombasa imeweka mikakati kabambe kuhakikisha wawekezaji wa sekta ya utalii wanakombolewa kutoka changamoto za kibiashara,” akasema Bi Asha Abdi, kaimu afisa mkuu wa Biashara na Utalii.

Bi Abdi alisema mipango hiyo itawasaidia kukabiliana na hali ngumu ya maisha hususan kibiashara.

Alisema Bunge la Kaunti ya Mombasa litafanya mageuzi katika Mswada wa Fedha ili kuhakikisha ada wanazotozwa hususan hoteli na mikahawa zinapunguzwa maradufu.

Alisema pia itahakikisha wanafanya kampeni ya kusaka soko la utalii wa humu nchini raia waweze kuzuru mji wa kitalii wa Mombasa.

“Katika kampeni hiyo tunawaambia wale waliokuwa wanapania kuzuru Mombasa wasisitishe ratiba yao badala yake wabadilishe tu tarehe na mambo yatakaporejea sawa wamiminike mji huu,” alisema Bi Abdi.

Bi Asha Abdi kaimu afisa wa Utalii na Biashara akizungumzia mpango wa serikali ya Kaunti ya Mombasa kuwasaidia wawekezaji katika sekta ya utalii kuimarisha biashara zao. Picha/ Winnie Atieno

Hata hivyo, alifichua itachukua muda kabla sekta hiyo kuimarika tena kutokana na virusi vya corona.

Bi Abdi aliwahakikishia wawekezaji hao kwamba watawaunga mkono ili wafufue sekta hiyo.

Serikali ya kaunti ya Mombasa ilichukua jukumu la kusaidia zaidi ya maredeva 120 waliokuwa wakifanya shughuli za kusafirisha watalii sehemu kadha wa kadha ikiwemo mbuga za wanyama.

“Sekta hii iliathirika kabla hata ya Kenya kuthibitisha kisa cha kwanza cha corona ambapo tulipoteza wageni kutoka kwa soko letu kuu ikiwemo Amerika, Barani Asia na Italia ambazo ziliathiriwa pakubwa na janga hili,” alisema Bw Innocent Mugabe aliyekuwa akisimamia ugavi wa chakula hicho.

Amesema kaunti imechukua hatua hiyo kusaidia madereva hao ili wajimudu hadi pale mambo yatakapokuwa shwari.

You can share this post!

Kitoweo cha samaki chajileta Garsen lakini hakuna ugali

Madereva kutoka Kenya wadai wanawekwa katika vituo duni vya...

adminleo