• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
KURUNZI YA PWANI: Shirika lawataka wanaojiuza kimwili waanze kuuza sabuni

KURUNZI YA PWANI: Shirika lawataka wanaojiuza kimwili waanze kuuza sabuni

Na MISHI GONGO

SHIRIKA la kijamii la Nkoko Iju Africa linapanga kuwafaidi makahaba 4,000 mjini Mombasa kwa kuwapatia ujuzi utakaowawezesha kujipatia mkate wao wa kila siku badala ya kujiuza kimwili.

Mradi huo unalenga kunufaisha asilimia 90 ya makahaba waliyopoteza ajira kufuatia kuzuka kwa ugonjwa wa Covid-19.

Akizungumza na wanahabari mjini Mombasa katika uzinduzi wa mradi huo Jumatano, mkurugenzi mtendaji katika shirika hilo Bi Maryland Laini alisema kufungwa kwa vilabu vya burudani na mikahawa ili kudhibiti kuenea kwa virusi vya corona kumewaathiri makahaba pakubwa.

“Makahaba hupata wateja wao katika sehemu hizi, lakini tangu kuwekwa kwa marufuku ya kutembea baada ya saa moja usiku na kufungwa kwa sehemu hizo, uchumi wa kundi hilo umepata pigo kubwa,” akasema.

Mradi uliozinduliwa unalenga kuwapa makahaba hao ujuzi wa kutengeneza sabuni na maziwa kutokana na maharagwe ya soya; bidhaa ambazo watauza ili kujipatia riziki.

Bi Laini alisema mradi huo unawalenga makahaba na wanawake walioachiwa majukumu ya kulea watoto wao.

Aliongezea kuwa kuwekwa marufuku ya kuingia na kutoka katika baadhi ya kaunti pia kunawazuia makahaba kukutana na wateja wao.

Alisema kufuatia kudorora kwa biashara hiyo makahaba wamelazimika kutoza wateja wao Sh20 kuwapa huduma kinyume na hapo awali ambapo waliwatoza Sh50 hadi 10,000 kutegemea na umri, sehemu waliyokutana na mambo mengine.

Mkurugenzi mtendaji katika shirika la Nkoko Inju Africa (kushoto) Bi Maryland Laini akiwa na baadhi ya makahaba walionufaika. Picha/ Mishi Gongo

Mbali na kuwapa ujuzi huo, pia watawaelimisha kuhusu haki zao za kikatiba.

“Tumeona makahaba wakinyanyaswa na wateja na hata maafisa wa polisi bila ya wao kuripoti matukio haya kwa kuchelea kutiwa mbaroni, katika mradi huu tutawafunza kuhusiana na haki zao,” akasema.

Alisema katika eneo la Nyali pekee kuna makahaba 2,900 huku Kisauni ikiwa na makahaba takriban 2,000.

“Kufuatia kufungwa kwa shule, idadi ya makahaba inaongezeka. Watoto wanapopata mimba za mapema huingilia ukahaba ili kujimudu wao na watoto wao,” akasema.

Mmoja wa wanachama katika shirika hilo Bi Elizabeth Mbuli aliiomba serikali kuwajumuisha makahaba katika mradi wa chakula unaolenga familia zisizojiweza.

Aidha aliwahimiza wanawake kuunda vyama ili kujiendeleza kiuchumi.

Bi Mbodze Katana ambaye ni mmoja wa waliofaidika na mradi huo alisema tangu janga la Covid-19 makahaba wengi wanashindwa kumudu mahitaji yao.

Alisema kuna baadhi ambao wanahitaji dawa za kupunguza makali ya Ukimwi lakini kufuatia hali ngumu ya maisha, wanashindwa kununua dawa hizo.

“Tunahofia kufa na makali ya njaa. Tunaomba serikali kutupa msaada wa chakula,” akasema.

Awali makahaba hao waliomba serikali kuwaorodhesha katika kundi la watu wanaotoa huduma muhimu.

You can share this post!

Mawakili walaumu mahakama kwa kupanga kutupa maelfu ya kesi

COVID-19: Visa jumla nchini Kenya vyafika 1,745

adminleo