• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 4:36 PM
Kicheko mahabusu kumlilia hakimu aongezwe ugali rumande

Kicheko mahabusu kumlilia hakimu aongezwe ugali rumande

TITUS OMINDE na BRIAN OCHARO

MAHABUSU aliye katika rumande ya Gereza Kuu la Elodret alisababisha kicheko mahakamani Jumatano alipodai kuwa maisha yake yamo hatarini kutokana na kipimo kidogo cha ugali ambacho anapewa kizuizini.

David Shikoli ambaye anakabiliwa na mashtaka ya kubaka mwanamke, alimwambia Hakimu Mkuu, Bw Harrison Barasa kuwa mwili wake unaendelea kudhoohofika kutokana na ugali mdogo anaopewa huko.

“Mheshimiwa huu mwili wangu haukuwa hivi. Nimepungua kutokana na chakula kidogo ambacho napewa kule jela. Sikuzoea maisha ya kula ugali kidogo. Tafadhali nitetee,” akasema Shikoli.

Aliiambia mahakama kuwa juhudi zake za kutaka kusikizwa na wasimamizi wa gereza hilo zimegonga mwamba, kwani maafisa husika wamekuwa wakimwambia kuwa jela si nyumba ya mama yake.

Hata hivyo, hakimu alimshauri awasilishe malalamishi yake kwa maafisa wa maslahi kutoka katika idara ya mahakama, ambao watazuru gereza hilo mwishoni mwa juma hili.

Shikoli alishtakiwa pamoja na wenzake ambao hawako mahakamani kwa kubaka mwanamke mmoja mnamo Desemba 23, 2017 katika kijiji cha Kambi Miwa kwenye kaunti ya Uasin Gishu.

Kesi yake itasikizwa Mei 7.

Katika mahakama ya Mombasa, mwanamume aliwaacha watu vinywa wazi, alipokiri kuiba vijiko 108 vya thamani ya sh3,780 kutoka duka kuu la Uchumi.

Theophilus Mutunkei Sakaya hata hivyo hakufafanua sababu za kitendo hicho.

Alishtakiwa kuiba vijiko hivyo kutoka kwa duka hilo kwenye barabara ya Moi mnamo Aprili 21 mwaka huu.

Hata hivyo, Sakaya aliachiliwa na Hakimu Mkazi Mkuu, Edgar Kagoni baada ya kusema kuwa alitaka kwenda kwa mazishi ya mama yake ambaye alikufa wiki moja iliyopita.

“Nimesikia malilio ya mshukiwa na kuzingatia kwamba vijiko vyote vimepatikana, nitamuachilia huru chini ya kifungu cha 35 cha Kanuni ya Adhabu ya Jinai,” alisema Bw Kagoni.

Inasemekana kwamba siku hiyo, Sakaya aliingia katika duka hilo saa tatu na nusu asubuhi akijifanya kuwa mteja.

Ripoti za polisi zasema alielekea moja kwa moja kwenye rafu ambapo vijiko vilikuwa na kuchukua rundo tisa za vijiko na kuziweka katika mfuko wake wa mbele.
 

You can share this post!

Lazima tuibadilishe Katiba hii – Raila

Majambazi wanawake ‘Wakware Babies’ waibuka...

adminleo