• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Mwili wa mwanamke aliyetoweka wapatwa umezikwa shambani

Mwili wa mwanamke aliyetoweka wapatwa umezikwa shambani

Na PETER NJERU

MWILI wa mwanamke aliyepotea kwa karibu wiki moja ulipatikana Jumapili ukiwa umezikwa kwenye shamba la mahindi katika eneo la Magutuni kaunti ya Tharaka-Nithi. 

Mwili huo uliokuwa umeanza kuoza uligunduliwa na mmiliki wa shamba hilo, ambaye alipiga ripoti kwenye kituo cha polisi cha Ntumu na maafisa wa polisi wakauchukua na kupeleka katika chumba cha kuhifadhi maiti cha hospitali ya rufaa ya Chuka.

Afisa mkuu wa polisi wilayani Chuka/Igambang’ombe Bw Barasa Sayia aliiambia Taifa Leo kuwa polisi wameanzisha uchunguzi juu ya tukio hilo.

“Polisi walichukua mwili na kupeleka katika chumba cha kuhifadhi maiti na wakaanzisha uchunguzi mara moja,” alisema Bw Sayia.

Tukio hilo la mauaji liliwaghadhabisha  wakazi ambao waliomba polisi kufanya uchunguzi wa kina na kumkamata muuaji.

Bw John Kithinji, momoja wa wakakijiji aliwaambia waandishi wa habari kuwa mtu anayejulikana na wenyeji kama, Bw Mutembei alikuwa mtuhumiwa wao mkuu.

“Mwanamke huyu amekuwa akihishi katika chumba kimoja na Bw Mutembei na kwa wiki moja iliyopita, wawili hao hawajaonekana,” alisema Bw Kithinji.

Bi Mary Gatwiri, mwanakijiji mwingine alisema usiku wa Jumatatu ya wiki jana, walisikia kelele iliyokuwa ikitoka  kwenye chumba ambacho marehemu aliishi na mtu huyo na asubuhi iliyofuata, wawili hao hawakuonekana.

Wakazi hao walilalama kuwa watu wengi wameuawa katika eneo hilo kwa kipindi cha miezi michache iliyopita na wakaomba polisi kuongeza usalama.

Aidha, wakaazi walisema kuongezeka kwa matumizi ya pombe haramu kwenye eneo hilo ni swala ambalo limechangia pakubwa kuongezeka kwa uharifu.

“Eneo hili linauzwa haina zote za pombe haramu na madawa wa kulevya sanasana bhangi,” alisema Bw Julius Mugendi, mwenyeji mwingine.

 

You can share this post!

Jombi ageuzwa gumzo mtaani kwa kuoa ajuza

Pwani yaapa kujisuka upya kuingia serikalini 2022

adminleo