• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 3:04 PM
Mvua yazuia mashahidi wa kesi ya Konza City kufika kortini

Mvua yazuia mashahidi wa kesi ya Konza City kufika kortini

Wakurugenzi wa kampuni ya mashamba ya Malili, kaunti ya Makueni wakiwa kizimbani Jumatatu. Picha/ Richard Munguti

Na RICHARD MUNGUTI

MASHAHIDI wanne waliokuwa wanatarajiwa kutoa ushahidi katika kesi ya wizi wa Sh553 milioni za mauzo ya ekari 5000 za shamba la Malili, kaunti ya Makueni ambapo kutajengwa jiji la Konza Techno dhidi ya wakurugenzi wanne wa kampuni ya Malili Ranch Limited (MRL) hawakufika kortini Jumatatu kwa sababu ya mvua iliyonyesha.

Kiongozi wa mashtaka Bi Lilian Obuor alimweleza hakimu mwandamizi Bw Lawrence Mugambi kwamba polisi waliwakuwa wamewapelekea samanzi mashahidi saba kufika kortini kutoa ushahidi wa Mabw David Ndolo Ngilai, James Kituku Munguti,Leonard Kyania Kitua na Julius Mbau Nzyuko.

“Ni mashahidi watatu tu waliofaulu kufika kortini kutoa ushahidi, wanne walikumbwa na matatizo ya usafiri kwa sababu ya mvua kubwa inayoendelea kunyesha kaunti ya Makueni,” Bi Obuor alisema kortini.

Kiongozi huyo wa mashtaka  aliambia mahakama mashahidi 60 wameandikisha  taarifa kwa polisi wakieleza jinsi wakurugenzi wa MRL waliiuzia Serikali ekari 5,000 kupitia kwa Wizara ya Habari na Mawasiliano bila idhini ya wenye hisa.

Serikali ililipa MRL Sh1,000,000,000 kupitia kwa wakili Eric Mutua.

Bi Obuor alimweleza hakimu  kuwa atafanya mashauri na maafisa wa polisi waliochunguza kesi hiyo waafikiano idadi ya mashahidi watakaoitwa kwa vile wote wanazugumzia suala moja.

Akitoa ushahidi mwanahisa wa MRL Bw Joseph Kavoo alisema alifahamishwa na mwanahisa mwenzake kuwa shamba alililogawiwa la ekari 7.8 liliuziwa Serikali na “wanahitajika kufika katika afisi ya Bw Mutua achukue hundi ya Sh1.1 milioni.”

Bw Kavoo alisema alifululiza hadi afisini mwa Bw Mutua na kupokea hundi ya Sh1.1milioni.

“Je, malalamishi yako ni nini dhidi ya wakurugenzi hawa wanne?” Bi Obuor alimwuliza Bw Kavoo.

“Shida yangu ni kwamba  wakurugenzi wa MRL hawakuwaita wenye hisa wapitishe hoja ya kuuzwa kwa ekari 5,000,” alijibu Bw Kavoo na kuongeza , “Wanahisa wengine walikuwa wanalipwa Sh1.4 milioni na zaidi lakini mimi nilipewa Sh1.1 milioni. Mwenye kupokea pesa kutoka kwa Serikali anatakiwa anilipe kiasi nilichostahili kulipwa.”

“Je, ulipokea pesa kutoka kwa washtakiwa hawa?” “Hapana.”

Wakurugenzi hao wamekanusha mashtaka ya wizi na kukaidi maadili ya afisi yao kwa kuruhusu kuuzwa kwa ekari 5,000  za shamba la MRL bila idhini ya wanahisa.

Kesi itaendelea Mei 15, 2018.

You can share this post!

Mabadiliko ya sheria ya SRC yaibua hofu

HISTORIA: Kenya kutuma setlaiti ya kwanza kwenye sayari

adminleo