• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Wanaosaka ajira ughaibuni watahadharishwa dhidi ya ugaidi

Wanaosaka ajira ughaibuni watahadharishwa dhidi ya ugaidi

Na WINNIE OTIENO

WAKENYA wanaotafuta kazi ng’ambo wametahadharishwa kuwa makini na kampuni zinazotumia nafasi hiyo kusajili watu kujiunga na makundi ya kigaidi.

Waziri wa Leba, Bw Ukur Yatani, aliwahatadharisha Wakenya kuwa makini na kampuni hizo akisema wizara yake imeidhinisha na kusajili kampuni 65 pekee za kibinafsi ambazo zimepewa idhini ya kuwaajiri Wakenya kufanya kazi ughaibuni.

Aidha alisema serikali imeanza kuchunguza kampuni zinazoshukiwa kuhusika na ulanguzi wa binadamu humu nchini.

Kwa muda sasa kampuni za kusajili Wakenya kufanya kazi ughaibuni zimelaumiwa kwa ulanguzi wa binadamu hususan kujiunga na kundi la kigaidi la ISIS nchini Syria.

Wiki iliyopita, jeshi la humu nchini liliwaokoa vijana 13 waliosajiliwa kujiunga na kundi la kigaidi la Al-Shabaab Somalia.

Akiongea Jumamosi alipokutana na baadhi ya wamiliki wa kampuni hizo eneo la Pwani, Bw Yatani aliwahakikishia Wakenya kuwa wizara yake itakabiliana na kampuni ghushi zinazoshukiwa kuwasajili wananchi kwenye makundi ya kigaidi.

“Kuna kanuni mpya za kuajiri Wakenya kwenda kufanya kazi ughaibuni. Ni sikitiko kuwa kampuni nyingi zinafuata kanuni lakini za huku Pwani hazifuati,” akasema waziri huyo katika Hoteli ya Sarova Whitesands.

Aliongeza: “Yale yanayotendeka si hadithi tunazozisoma au kuona kwenye runinga. Imefanyika  nchini mwetu. Kuna ulanguzi wa watu katika maeneo yasiyojulikana na ni lazima tuwe makini. Tunasihi kampuni za kusajili Wakenya kutupasha habari kuhusu kampuni ghushi ama zinazoshukiwa.”

Alilaumu kampuni ghushi kwa masaibu ambayo Wakenya wngi wanapitia wanapoenda kufanya kazi Uarabuni.

“Tusidanganyane kwani Wakenya wanateseka sana huko Uarabuni. Lakini ni sharti tuhakikishe hawateseki wanaposafiri nchi hizo. Maisha ya Wakenya ni muhimu sana lazima walindwe,” akasema.

 

 

 

You can share this post!

Prof Ghai ataka fedha zilizotumika na Jubilee Ikulu ziwekwe...

Ford Kenya na ANC wakosa kuafikiana

adminleo