• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 6:55 AM
Wito serikali ibuni sera ya kuruhusu ndege kupaa na kutua uwanja wa Moi bila vikwazo

Wito serikali ibuni sera ya kuruhusu ndege kupaa na kutua uwanja wa Moi bila vikwazo

Na WINNIE ATIENO

WAWEKEZAJI katika sekta ya utalii wametoa wito kwa serikali ikubali sera inayoruhusu ndege kutua na kupaa katika uwanja wa ndege wa Moi moja kwa moja bila vikwazo.

Wawekezaji hao walisema sera hizo zitasaidia kufufua sekta ya utalii ambayo inaendelea kuzorota kufuatia janga la corona.

Hata hivyo walisisitiza kuwa ndege za moja kwa moja uwanja huo zitasaidia kukuza sekta nyingi ikiwemo ile ya utalii, biashara na uchukuzi hivyo basi kufungua ajira miongoni mwa wakenya.

“Watu wengi hupenda usafiri bila changamoto, serikali inafaa kukubali sera inayoruhusu ndege kutua na kupaa katika uwanja wa ndege wa Moi moja kwa moja bila vikwazo” alisema Bw Husnain Noorani kwenye mahojiano.

Akiongea kwa niaba ya wawekezaji wa sekta ya utalii na wamiliki wa hoteli za kifahari, Bw Noorani aliitaka serikali kuhakikisha bodi ya utalii nchini inafadhiliwa ili kuuza soko la Kenya kama kituo maalum cha utalii duniani.

Alisema endapo serikali itakubali sera hiyo, ndege nyingi zitapaa na kutua katika uwanja wa kimataifa wa ndege ya Moi na kuimarisha uchukuzi, utalii na biashara.

Uwanja huo ndio mkubwa zaidi sehemu ya Pwani.

Kwa upande wake, mwenyekiti wa muungano wa wawekezaji wa utalii Bw Ishpal Oberoi, alisema biashara katika uwanja huo wa ndege unaweza kupigwa jeki endapo ndege zitakuwa zinapaa na kutua moja kwa moja.

“Kama tunataka kukuza eneo la Pwani kama soko la utalii, ni sharti tuweke mikakati kabambe ikiwemo kuhakikisha ndege zinatua na kupaa bila vikwazo. Ndege za kimataifa kutoka bara Uropa, Amerika na hata Asia zinaweza kuleta wageni,” alisema.

Bw Oberoi ambaye pia ni mkurugenzi wa kampuni maarufu ya kusafirisha watalii ya Kuldip, alisema sekta hiyo imeanza kuimarika hasa maeneo ya Diani, Kilifi, na Maasai Mara.

Hata hivyo alisema kuna matumaini ya utalii kuimarika kaunti ya Mombasa wakati wa likizo ya Agosti.

Lakini Waziri wa Utalii na Wanyama wa porini Bw Najib Balala alisema serikali itaweka mikakati kuhakikisha ndege za kimataifa zinatua uwanja huo.

“Ni dhahiri uchumi wa utalii umezorota duniani na kila mtu anaogopa. Kwa mfano barani Uropa, hakuna ndege ya inayokwenda Marekani sababu ya wasiwasi dhidi ya kuambukizwa virusi hivi. Tunaweka mipango ili uwanja huo upate ndege za kimataifa. Tuna Rwanda Air, Turkish Airways, Qatar Airways na Ethiopian Airways lakini tunataka ndege nyingine zisafirishe wageni Mombasa ili kukuza sekta hiyo,” alisema kwenye mahojiano wiki iliyopita.

Hata hivyo aliwataka wakenya kupiga jeki utalii wa humu nchini ili kufufua uchumi.

You can share this post!

CORONA: Watu 23 wafariki

Wapinzani waenda mafichoni wakihofia kunaswa na serikali

adminleo