• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 8:12 PM
Madaktari washinikiza kupewa bima ya afya

Madaktari washinikiza kupewa bima ya afya

JUMA NAMLOLA na WINNIE ATIENO

MADAKTARI katika hospitali za umma Kaunti ya Mombasa, sasa wanataka serikali iwape bima ya afya huku visa vya maambukizi nchini vikifika 22,053.

Ingawa Mombasa ilikuwa na kisa kimoja pekee kati ya watu 690 walioambukizwa kote nchini jana, madaktari wanaotibu wagonjwa wa corona walisema wako katika hatari kubwa ya kuambukizwa, ilhali hawana bima ya afya.

“Ni kinaya kwamba madaktari katika kaunti hii hawana bima ya afya, hata baada ya kujitolea kusaidia nchi kukabiliana na janga hili la corona,” alisema Dkt Abidan Mwachi, mwakilishi wa Pwani katika chama cha KMPDU.

Alisema kukosekana kwa bima ya afya ni hatari ambayo wahudumu wa afya wanakodolea macho, hasa wakati huu ambapo tayari wahudumu 45 wameambukizwa virusi hivyo wakiwa kazini.

Dkt Mwachi alimsihi Gavana Hassan Joho na Hazina ya Taifa ya Bima ya Afya (NHIF) kutatua jambo hilo, ili wahudumu wa afya waweze kupata huduma hiyo muhimu

.“Mgogoro ulioko kati ya NHIF na serikali ya Kaunti ya Mombasa unafaa kutatuliwa haraka iwezekanavyo ili wahudumu wa afya waweze kuwekwa kwenye bima hiyo ya afya,” alisema Dkt Mwachi.

Pia chama hicho cha KMPDU kilitoa wito kwa serikali za kaunti kuhakikisha wahudumu wa afya wanapewa barakoa maalum za N95 ili kujikinga dhidi ya virusi hivyo.

“Barakoa za N95 ndizo zinazofaa kutumiwa na wahudumu wa afya katika janga hili. Pia tunaonya Wakenya dhidi ya unyanyapaa miongoni mwa watu wanaouguza virusi vya corona,” alisisitiza Dkt Mwachi.

Kaunti ya Mombasa bado ni ya pili kwa maambukizi ikiwa na watu 2,067 baada ya mtu mmoja kuambukizwa jana.

Nairobi jana iliongoza kwa visa 535 na kufanya idadi ya watu wote walioambukizwa katika kaunti hiyo kuwa 13,416, ambayo ni zaidi ya nusu ya maambukizi yote nchini.

Idadi ya wagonjwa walioruhusiwa kuondoka hospitalini na karantini pia iliongezeka kwa watu 58 huku watu watano wakiaga dunia.

You can share this post!

TAHARIRI: Pendekezo la vyuo laonyesha ubinafsi

Nitatoa ushahidi tume ya kuchunguza kifo cha Msando...

adminleo