• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 3:25 PM
Joho sasa aamua kushirikiana na Uhuru

Joho sasa aamua kushirikiana na Uhuru

MOHAMED AHMED Na VALENTINE OBARA

GAVANA wa Mombasa, Hassan Joho, hatimaye amelegeza kamba na kutangaza atashirikiana na serikali ya Rais Uhuru Kenyatta.

Haya ni mabadiliko makubwa ya msimamo wake mkali ambao ameshikilia kwa muda mrefu dhidi ya utawala wa Rais Kenyatta na naibu wake William Ruto. Ni kutokana na msimamo huo na ukakamavu wa kushambulia wawili hao ambapo gavana huyo amepata umaarufu kitaifa.

Lakini jana akizungumza katika eneo la Shanzu mjini Mombasa alipoongoza hafla ya upandaji miti, naibu kiongozi huyo wa Chama cha ODM alionekana kushawishika kwamba serikali haina ubaya naye.

“Nataka kusema hapa kuwa tuna furaha kufanya kazi na serikali ya kitaifa kwa sababu ni kupitia njia hiyo ambapo watu wetu watapata nafasi ya kufaidika kimaendeleo,” akasema.

Alitamka hayo mbele ya viongozi wa Jubilee, Maseneta Kimani Wamatangi (Kiambu), Charles Kibiru (Kirinyaga) na Millicent Omanga (Seneta Maalum).

Bw Wamatangi aliongoza wenzake kumwomba Bw Joho aweke kando tofauti zake na serikali kuu na kufuata mfano uliotolewa na Rais Kenyatta na kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga kwa manufaa ya wananchi.

“Viongozi wa Jubilee ni wema na tunataka kuhakikisha tunaleta umoja. Ninataka kumwambia Bw Joho anapoongoza kaunti, anafaa kushirikisha kila mmoja ili tufanye kazi pamoja,” akasema Bw Wamatangi.

Kufuatia wito huo, Bw Joho alisema: “Tumeona kuwa wadosi wetu wamesalimiana, wakashikana mkono. Mimi mdosi wangu ni Bw Raila na hivyo basi tutawaunga mkono na tutaendelea kuwaunga mkono.”

Uhasama kati ya Bw Joho na Rais Kenyatta ulichacha wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka uliopita, ambapo ilibidi serikali itumie polisi kumzuilia kuhudhuria baadhi ya hafla zilizosimamiwa na rais Mombasa.

Matukio yaliyojaa vioja zaidi yalikuwa wakati polisi walipozuia msafara wake asihudhurie uzinduzi wa kituo cha reli mpya ya SGR kilicho Miritini, na uzinduzi wa feri mpya ya Mtongwe.

Rais Kenyatta alidhihirisha ghadhabu yake dhidi ya Bw Joho alipokuwa Mtongwe ambapo alimtaka akome kumfuata kila aendako. “Tunafuatana naye kufanya nini? Mimi sio bibi yake na sina haja naye.

Atekeleze shughuli zake kama anazo, lakini shida yake ni kwamba hakuna lolote ametenda ndiposa anataka kuja kushikilia koti ya serikali ya kitaifa,” akasema rais katika hafla hiyo ya Machi 2017.

Bw Joho amekuwa akipinga hatua ya serikali kuu kujenga bandari kavu katika maeneo ya Embakasi jijini Nairobi na Naivasha katika Kaunti ya Nakuru akidai kwamba mipango hiyo itaathiri uchumi wa Pwani ambao hutegemea sana biashara za Bandari ya Mombasa.

You can share this post!

Mabao 31 yavumwa siku ya mwisho ya EPL, Salah avunja rekodi

Mke akamatwa baada ya mwili wa mume kupatikana kwenye buti

adminleo