• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 5:22 PM
‘Tangatanga’ wawekea DCI na EACC presha

‘Tangatanga’ wawekea DCI na EACC presha

Na MISHI GONGO

KUNDI la wanasiasa wa mrengo wa ‘Tangatanga’ limemtaka mkurugenzi wa idara ya uchunguzi wa makosa ya jinai (DCI) na maafisa wa tume ya maadili na kupambana na ufisadi (EACC) kukoma kuwahangaisha wafuasi wa Naibu Rais William Ruto na badala kuwakamata waliyohusika katika sakata ya pesa za corona.

Wakizungumza katika shule ya msingi ya Kongowea mjini Mombasa katika hafla ya kuwakabidhi wazee kadi za bima ya afya, ambayo ilihudhuriwa na Naibu Rais William Ruto, viongozi hao wamesema japo majina ya walioshiriki katika wizi huo yametolewa parawanja, maafisa hao hawajawachukulia hatua yoyote.

Wakiongozwa na mbunge wa Nyali Mohammed Ali, wamesema serikali imekuwa ikiwaandama wafuasi wa Dkt Ruto kama njia ya kuwaadhibu kwa msimamo wao.

“DCI na EACC waache kuwaandama kina Aisha Jumwa na wengineo. Tunataka bilioni zilizoibiwa katika sakata ya corona zirudishwe,” akasema mbunge huyo.

Mohammed Ali aliyekuwa amevaa maski akiingia kwa mkutano huo amesema hatovaa maski hadi pale pesa zilizoibwa zitakaporudishwa.

Naibu Rais William Ruto akihutubia umati. Picha/ Mishi Gongo

Aidha wameutia dosari mpango wa maridhiano (BBI) wakisema kuwa ni njama ya aliyekuwa waziri mkuu Raila Odinga na Rais Uhuru Kenyatta ‘kujinufaisha’.

“Hii ni kutaka kuleta ukabila katika serikali. Wanataka kupata vyeo hata ikitokea wameangushwa debeni na kuwafanya walipa ushuru kugharimia umero wao,” akasema.

Mbunge huyo alisema hata baada ya mageuzi yaliyoleta Katiba Mpya mwaka 2010 eneo la Pwani bado limesalia nyuma kimaendeleo.

Alisema kufikia sasa Wapwani wengi bado wanaishi kama maskwota kwa kukosa hatimiliki za vipande vya ardhi.

You can share this post!

Chelsea wamsajili beki Thiago Silva kutoka PSG

Visa vya utapiamlo vyaongezeka Mombasa