• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Serikali yasaka Sh100 bilioni kufufua biashara

Serikali yasaka Sh100 bilioni kufufua biashara

Na VALENTINE OBARA

SERIKALI inalenga kupata angalau Sh100 bilioni za kutoa mikopo kwa wafanyabiashara wadogo.

Serikali Alhamisi ilitangaza kubuni hazina ya kutoa mikopo kwa wafanyabiashara wadogo hasa walioathiriwa na makali ya janga la corona.

Katika kikao cha Baraza la Mawaziri kilichofanywa jana katika Ikulu ya Nairobi, serikali iliamua kuweka kitita cha Sh10 bilioni kwenye hazina hiyo.

Jumla ya Sh5 bilioni zitawekwa katika kipindi cha fedha cha mwaka huu, huku Sh5 bilioni nyingine zikiongezwa katika mwaka wa fedha wa 2021/2022, kwa mujibu wa taarifa kutoka Ikulu.

Mkutano wa jana ulioongozwa na Rais Uhuru Kenyatta ulihudhuriwa pia na Naibu Rais William Ruto.

Serikali ilisema inatarajia hazina hiyo itapokea fedha zaidi kutoka kwa mashirika ya kifedha yanayojihusisha na masuala ya ustawishaji wa maendeleo, na mabenki ya kibinafsi lengo likiwa ni kufikisha Sh100 bilioni.

“Inatarajiwa hazina hii itaanza kutumiwa ifikapo katikati ya Oktoba, 2020,” Ikulu ikasema.

Maelfu ya wafanyabiashara kote nchini walipata pigo tangu janga la corona lilipothibitishwa nchini mnamo Machi, hadi wengi wao wakalazimika kufunga biashara zao.

Hali hii ilichochewa sana na kanuni kali zilizotolewa nchini na ulimwenguni kote katika juhudi za kuepusha ueneaji wa maambukizi ya virusi vya corona.

Wakati huo huo, mpango wa kuboresha makao katika mtaa wa mabanda wa Mukuru, Kaunti ya Nairobi, ulipiga hatua baada ya Baraza la Mawaziri kuidhinisha utekelezaji wake.

Nyumba

Mradi huo utakaogharimu takriban Sh15 bilioni unalenga kujenga nyumba 13,000 za bei nafuu.

Utatekelezwa kwa ushirikiano na wawekezaji wa kibinafsi.

Ujenzi wa nyumba za bei nafuu ni mojawapo ya malengo makuu ambayo Rais Kenyatta amenuia kufanikisha kabla astaafu urais kikatiba ifikapo mwaka wa 2022.

Malengo mengine kati ya manne ambayo Jubilee ilinuia kutekeleza katika kipindi hiki cha pili cha uongozi ni uboreshaji wa huduma za afya kwa bei nafuu, uzalishaji chakula cha kutosheleza mahitaji ya umma na ustawishaji viwanda.

Kikao cha jana kilikuwa cha kwanza tangu mawaziri walipokamilisha likizo ya wiki mbili mnamo Agosti 28.

You can share this post!

Mfano mbaya!

LISHE: Jinsi ya kutayarisha achari ya mbirimbi