• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 1:47 PM
Familia yataka ripoti ya daktari kuhusu mtoto wao aliyefariki

Familia yataka ripoti ya daktari kuhusu mtoto wao aliyefariki

Na SAMMY KIMATU

[email protected]

MTOTO wa umri wa miaka tisa alifariki Jumatano katika kisa chenye utata katika mtaa mmoja wa mabanda kaunti ya Nairobi.

Kisa hicho kilitokea mwendo wa saa kumi na moja za jioni katika mtaa wa mabanda wa Mukuru-Kayaba ulioko wodi ya Landi Mawe katika kaunti ndogo ya Starehe.

Polisi walitambua mtoto huyo kwa jina David Nyabera, mwanafunzi wa darasa la tano katika Shule ya Msingi ya Mukuru.

Kwa mujibu wa mamake marehemu, Bi Rose Nyanjama, 32, mwanawe alikuwa ameenda kwa kakake mkubwa akiambatana na dadake kabla ya kifo chake kutokea.

“Alikuwa mchangamfu. Tulishiriki naye chakula cha mchana na kisha nikamtuma kununua kuni za kupika chipsi, ‘’ Bi Nyanjama, mchuuzi wa vyakula mtaani humo akasema.

Aliongeza kwamba mtoto wake hajawahi kuwa na historia ya ugonjwa wowote wala hakuwa na dadili ya maradhi kabla ya kufariki.

Babake marehemu, Bw Charles Nyabera, 58 aliiambia Taifa Leo kwamba marehemu aliambatana na dadake kwenda kwa kakao mkubwa kumtembelea takribani mita 200 kutoka kwao.

“Aliondoka hapa kwetu eneo la Budalangi-Cluster ‘A’ na wakiwa ndani ya nyumba kwa kaka yao, akaanguka na kuzirai papo hapo,” Bw Charles asema.

David Nyabera, aliyekuwa mwanafunzi wa darasa la tano katika Shule ya Msingi ya Mukuru. PICHA/ SAMMY KIMATU

Majirani pamoja na mamake walipoarifiwa kuhusu tukio hilo, walimpeleka mwanafunzi huyo katika kliniki moja mtaani.

“Alikuwa akitokwa na pofu iliyochanganyika na damu kutoka mapuani na mdomoni. Tulijaribu kumpea huduma ya kwanza lakini akakata roho,” muuguzi katika zahanati akaeleza.

Msemaji wa familia hiyo ambaye kadhalika ni mwenyekiti wa bodi ya Shule ya Msingi ya Mukuru, Bw Peter Okari alisema watasubiri ripoti ya daktari wa upasuaji ili wabaini kilichosababisha kifo cha mwanao.

‘’Kama familia, hatutaki habari sisizo sahihi kuenezwa mtaani hadi pale daktari atatoa ripoti yake baada ya upasuaji wa mwili wa marehemu kufanyika,” Bw Okari akanena.

Akizungumza katika boma ya marehemu, mwenyekiti wa usalama katika mtaa huo, Bw Jacob Ibrahim aliwaonya wenyeji kutosabaza habari za uwongo kuhusu tukio hilo.

Vilevile, aliwashauri wazazi kuhakikisha wamewacha wanao wakiwa kwenye ulinzi wa watu wazima wanapoelekea maeneo tofauti kufanya kazi zao za kila siku.

“Watoto wako katika likizo ndefu kufuatia janga la Corona. Ni muhimu wazazi kuhakikisha watoto wao wako salama nyumbani kabla ya kuelekea kazini,” Bw Jacob akanena.

Maafisa wa polisi kutoka kituo cha polisi cha Industrial Area walipeleka mwili wa marehemu katika chumba cha kuhifadhi maiti cha City.

Mwaka huu, watoto wanne kutoka mtaa wa Mukuru wamefariki wakiwa nyumbani tangu shule zilipofungwa baada ya janga la corona kutangazwa nchini.

Katika kisa cha kwanza, mvulana wa darasa la saba aligongwa na gari katika barabara ya Entreprise, Eneo la Viwandani.

Fauka ya hayo, msichana wa kidato cha pili katika Shule ya upili ya St Michael alifariki akiwa maeneo ya mashambani katika Kaunti ndogo ya Mbooni East.

Isitoshe, mwanafunzi wa mwaka wa pili katika Our Lady of Mercy Vocational Training Centre aliuawa na raia kwa kushukiwa kuwa mhalifu katika mtaa huo.

Ripoti ya visa vyote hivyo ilitolewa kutoka ofisi kuu ya Mukuru Promotion Centre (MPC).

MPC ni shirika la misingi ya dini linaloendeshwa na Watawa wa Mercy kutoka Ireland (Irish Sisters of Mercy).

Kadhalika, MPC ndilo mdhamini rasmi wa shule ya Msingi ya Mukuru na ya Upili ya St Michael na Chuo cha Mafunzo ya Ufundi cha Our Lady of Mercy.

You can share this post!

ANA KWA ANA: Mshonaji aliyezamia katika kuwang’arisha...

Wachezaji mahiri lakini bado hawajashindia klabu zao taji