• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:05 AM
MAUYA O’MAUYA: Demokrasia ni kama rinda, kila taifa huvaa linaloifaa

MAUYA O’MAUYA: Demokrasia ni kama rinda, kila taifa huvaa linaloifaa

Na MAUYA O’MAUYA

Ukiona vyaelea vimeundwa. Ndivyo ilivyo kwa nchi ya Amerika katika masuala ya utawala wa Kidemokrasia tangu ilipojitwalia uhuru mwaka wa 1776.

Naam, inakanganya mawazo ya wengi kuwazia kwamba taifa la nguvu na ukwasi tunaoshuhudia sasa lilikuwa limekandamizwa na minyororo ya ukoloni. Chinua Achebe alinasihi kuhusu hili ‘Utazamapo domo la mfalme, huwezi kuamini naye aliwahi kunyonya matiti ya mamake’. Amerika ilitawaliwa na Uingereza.

Juma lililopita, raia wa dunia waligeuka wataalamu kutoa maoni, kuchanganua na kufuatilia uchaguzi wa Marekani. Hata kina yakhe wa kwetu madongokaporomakani wasiojua tofauti ya Washington na Washington DC walijitwika umahiri wa magwiji wa kuelezea mwelekeo wa mkwaruzano kati ya Donald Trump na Joe Biden.

Mwingine aliniatua mbavu kwa kudai Biden anafaa kwa sababu anaunga mkono BBI. Lahaula! Lililosalia kwetu hasa ni mafunzo muhimu kuhusu utawala wa demokrasia na uendeshaji wa chaguzi za uwazi. Isidhaniwe kwamba Amerika ni paradiso ya demokrasia duniani lakini ilivyo, ni heri nusu shari kuliko shari kamili.

Funzo moja kuu nitaluzungumzia ni usawa na kudumisha hadhi ya kila Jimbo na haki za raia wake. Hii inatokana na mfumo wa kuteua rais kupitia wajumbe 538 wa majimbo licha ya raia mamilioni kupiga kura ya moja kwa moja.

Takriban watu milioni 200 wana haki ya kupiga kura Marekani lakini mgao wa wajumbe 538 kwenye majimbo 50 ya Amerika ndio uamua kiongozi wa nchi.

Mgao huu umeundwa kwa misingi ya idadi ya watu na haja ya kuwakilishwa ili kila Jimbo liwe na sauti katika uchaguzi wa Rais. Demokrasia ni sawa na rinda, vaa linalokufaa.

Mfumo wa Amerika umewafaa kwa kuhakikisha kwamba majimbo yaliyo na idadi kubwa ya watu hayatasakama yale ya wachachache wanapochagua Rais.

Basi, jimbo la California lenye idadi ya watu milioni 40 linatoa wajumbe 55 huku Jimbo la Wyoming la watu nusu milioni likichangia wajumbe watatu kwa mshindi wa kura.

Kwa mtazamo usio makini ungedhani huu ni upuzi lakini ukipiga darubini utagundua mfumo huu ndio umehakikisha uwepo wa muungano wa majimbo 50 na umoja wa kitaifa wa Amerika kwa yakaribia miaka 245 sasa .

Ingekuwa demokrasia ya hesabu ya wingi wa watu pekee, Amerika ingesambaratika kwa sababu ya udikteta wa maslahi ya majimbo makubwa kama vile California, Texas au Florida.

Majimbo madogo yangekandamizwa na tungeshuhudia hata mapigano ya kujitenga au kutangaza uhuru wao. Ili kutwaa urais, kiongozi anahitaji kura za wajumbe 270 au zaidi kutoka majimbo ya nchi. Jinsi Ile kila mpiga kura ni muhimu, kila kura ya mjumbe ni muhimu na zaidi ya yote, kila jimbo ni muhimu.

Ukiwa mgombeaji aliye na kura za wajumbe 267 utahitaji uungwaji mkono na Jimbo kama vile Montana, Vermont, Delaware au Dakota Kaskazini ili kutwaa urais wa Amerika. Majimbo haya yana idadi ndogo ya watu na yanachangia wajumbe watatu kila moja. Haiwezekani kabisa viongozi wa kitaifa kupuuza matakwa ya kitengo cha jamii japo ni wachache.

Nchini Kenya vitengo vyetu vya kigatuzi ni Kaunti zetu 47. Kijamii tuna makundi kadha hasa kwa vigezo vya makabila, jinsia, umri, dini, rangi, wasiojiweza na kadhalika.

Mchango wao usipuuzwe katika uamuzi wa kuchagua utawala. Hata hivyo ni bayana kwamba hatujafaulu kukarabati mfumo wa uchaguzi wa Rais unaohakikisha kila kitengo kinawakishwa. Tumekwama kwenye tope la ukabila.

[email protected]

 

You can share this post!

Corona na ICC zimemtoa pumzi Ruto – Wadadisi

CECIL ODONGO: Utata wa BBI pia ulibugika miswada ya Bomas,...