• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Sitaomba msamaha, Magoha awaambia wakosoaji

Sitaomba msamaha, Magoha awaambia wakosoaji

Na LILLIAN MUTAVI

WAZIRI wa Elimu, Prof George Magoha, amesisitiza kwamba, hatabadilisha mtindo wake wa kufanya kazi, licha ya kutakiwa kuomba msamaha kuhusiana na kisa ambapo alinaswa akimkaripia afisa wa elimu.

Prof Magoha alinaswa kwenye video akimfokea vikali Mkurugenzi Mkuu wa Elimu katika Kaunti ya Uasin Gishu, Bw Gitonga Mbaka, katika Shule ya Msingi ya Langas wiki iliyopita.

Akiwahutubia wanahabari jana katika Shule ya Msingi ya Kyamutheke, Kaunti ya Machakos, Prof Magoha alisema baadhi ya maafisa wa elimu walio nyanjani wamekuwa wakizembea katika utekelezaji wa majukumu yao kwa hivyo mtindo anaotumia ndio unafaa ili wananchi wahudumiwe inavyotakikana.

“Watu hawapaswi kushangazwa na mtindo wangu wa kufanya kazi. Nilihudumu katika Baraza la Kitaifa la Mitihani Kenya (KNEC) ambako nililainisha mambo. Sasa niko hapa kuhakikisha mahitaji ya wazazi na wanafunzi yametimizwa wakati wowote ule. Ikiwa siwezi kufanya hivyo, basi sipaswi kuwepo kwenye wizara,” akasema.

Alisema baadhi ya wafanyakazi katika wizara hiyo hawalengi kutekeleza wajibu wao wa kuboresha sekta ya elimu kikamilifu.

Alieleza kuwa, baadhi ya maafisa walio nyanjani hawatembelei shule zilizo katika maeneo wanayosimamia, hivyo hawapaswi kupokea mishahara.

“Ikiwa unasimamia shule 30 katika eneo lako, ambapo kufikia mwishoni mwa mwezi hujatembelea hata shule kumi, hupaswi kupokea mshahara. Maafisa hao lazima wawajibikie majukumu yao, la sivyo nitawafanya kutimiza hayo. Tunapaswa kuwatendea haki watoto wetu kwani serikali inatumia fedha nyingi kutimiza maslahi yao,” akasema.

Wadau mbalimbali, wakiwemo maafisa wa vyama vya walimu, wamemkashifu waziri huyo hasa kwa maneno makali aliyotumia dhidi ya afisa huyo wa elimu.

Baadhi yao walimtaka aombe msamaha, la sivyo wawasilishe ombi kwa Rais Uhuru Kenyatta ili asimamishwe kazi kwa madai ya kukosa maadili.

Prof Magoha amejipata taabani kwa muda sasa, kwani amekuwa akikashifiwa pia kwa jinsi anavyosimamia sekta ya elimu wakati wa janga la corona. Baadhi ya wazazi na walimu hudai kukanganywa na matamshi yake.

Kuhusu suala la uwepo wa madawati shuleni, alisema kufikia sasa wamesambaza vifaa hivyo kwa zaidi ya robo tatu ya shule za msingi na upili nchini. Haya hivyo, alisema Machakos bado haijapokea madawati hayo ipasavyo.

You can share this post!

Je, chama cha wilibaro kitasajiliwa?

Pfizer inajuaje nitapata virusi vya corona? – Kagwe