• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 6:50 PM
Dawa bandia za hamu ya mapenzi zinavyohatarisha maisha ya wanaume

Dawa bandia za hamu ya mapenzi zinavyohatarisha maisha ya wanaume

NA PAULINE ONGAJI

 

WANAUME humu nchini wamekuwa wakihatarisha maisha yao kwa kutumia kiholela dawa za kuongeza hamu ya mapenzi au nguvu za kiume.

Uchunguzi uliofanywa na mamlaka ya kudhibiti ubora wa vyakula na dawa nchini Amerika (FDA) ulibaini kuwa nyingi ya dawa za kuongeza hamu ya mapenzi au nguvu za kiume ambazo zimekuwa zikiuzwa madukani na mitandaoni ni hatari kwa afya.

Mamlaka hiyo, wiki iliyopita, ilitoa orodha ya zaidi ya dawa 50 za kuongeza hamu ya mapenzi na kupunguza uzito zilizo na viungo fiche ambavyo vinaweza kuhatarisha maisha haswa miongoni mwa watu ambao wanatumia dawa za kisukari, presha, maradhi ya moyo, nakadhalika.

Baadhi ya dawa zilizo katika orodha hiyo zimekuwa zikiuzwa katika maduka na mitandao ya humu nchini hivyo kutia hatarini maisha ya maelfu ya wanaume ambao wamekuwa wakizitumia ili ‘kufurahisha’ wapenzi wao kitandani.

Mamlaka ya FDA ilinunua dawa hizo katika mitandao ya Amazon na eBay na baada ya kuzifanyia vipimo ilibaini kuwa zina viungo fiche ambavyo ni hatari kwa afya licha ya wauzaji wazo kudai kuwa ni salama.

Miongoni mwa tembe za kuongeza nguvu za kiume au hamu ya mapenzi zilizogunduliwa kuwa hatari kwa afya ni PremierZEN, U.S.A Viagra na Herb Viagra kati ya nyingine nyingi ambazo zimekuwa zikiuzwa madukani na mitandao ya humu nchini.

Kwa mfano, FDA ilibaini kuwa tembe zinazojulikana kama U.S.A Viagra zina kiungo kinachofahamika kama sildenafil ambacho hupatikana katika tembe ambazo hupewa wagonjwa walio na matatizo ya nguvu za kiume.

Tembe za Herb Viagra pia zilipatikana na kiungo hicho. Tembe za PremierZen zina viungo vya sildenafil na tadalafil ambazo hupatikana kwenye tembe za Viagra na Cialis ambazo zimeidhinishwa humu nchini kutumika kutibu wagonjwa walio na matatizo ya nguvu za kiume.

Japo tembe za Viagra na Cilialis zimeidhinishwa kutumika kutibu watu walio na matatizo ya nguvu za kiume, zimepigwa marufuku kuuzwa madukani – ni sharti zitumiwe chini ya usimamizi wa daktari aliyehitimu.

Tembe za PremierZen, kwa mfano, zinapatikana kwa urahisi mitandaoni na zinauzwa kwa kati ya Sh3,000 na Sh6,000 kulingana na idadi ya tembe.

Katika tovuti ya jiji.co.ke dawa ya Herb Viagra inauzwa kwa kati ya Sh2,000 na Sh4,000.Mafuta ya Beast yanayodai kumfanya mwanaume kuwa na nguvu za kiume kwa muda mrefu wakati wa kufanya mapenzi yanauzwa kwa Sh6,500 katika maduka mbalimbali nchini.

Mtandao wa G Spot Kenya, unauza mafuta ambayo unadai yanamwezesha mwanaume kuwa na nguvu za kiume kwa dakika 60. Mafuta hayo yanauzwa kwa Sh2,000.

Ripoti iliyotolewa na mtandao wa ePharmacy Kenya ilifichua kuwa tembe za kuongeza hamu ya mapenzi ni miongoni mwa dawa ambazo zinanunuliwa zaidi na Wakenya kupitia mitandaoni.

Wengi wanapendelea kununua dawa hizo kupitia mitandaoni ili kujificha.Watu wanaponunua dawa kupitia mitandaoni hupelekewa dawa hizo hadi nyumbani hivyo kuzitumia wanavyotaka bila kupata ushauri wa daktari.

Kulingana na Dkt Gitobu Mburugu, mtaalamu wa maradhi ya mfumo wa uzazi katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH), kuna aina tatu za dawa ambazo zimeidhinishwa kutumika kutibu wanaume walio na matatizo ya nguvu za kiume humu nchini.

Dawa hizo ni Viagra, Cialis na Vardenafil. Dawa hizo ni sharti zitolewe na daktari aliyehitimu na ni marufuku kuzinunua dukani.

Dawa ya Vardenafil inauzwa kwa kutumia majina ya Levitra, Vivanza na Staxyn.Dkt Mburugu anasema kuwa dawa feki zinazodai kuwa Viagra au Cialis zimejazana madukani ambazo huhatarisha maisha ya watumiaji wake.

Uchunguzi uliofanywa na kampuni ya Pfizer ambayo imetengeneza Viagra, ulionyesha kuwa asilimia 80 ya dawa zinazouzwa mitandaoni zikidai kuwa Viagra, ni feki.

Mnamo 2017, Bodi ya Dawa na Sumu nchini (PPB) ililalamikia kuhusu ongezeko la dawa ghushi zinazodai kuongeza hamu ya mapenzi au nguvu za kiume humu nchini.

Kulingana na mkurugenzi wa idara ya utekelezaji wa sheria kuhusu matumizi ya dawa wa PPB, Peter Mbwiiri Ikamati, tembe zinazodaiwa kuongeza hamu ya mapenzi ni miongoni mwa dawa zilizoghushiwa kwa wingi humu nchini.

Mnamo Agosti, mwaka huu, maafisa wa Idara ya Uchunguzi wa Uhalifu (DCI) walinasa mwanaume aliyepatikana akiuza tembe feki za Viagra katika mtaa wa Hurlingham, Nairobi.Kulingana na DCI, mshukiwa aliyetambuliwa kwa jina la Cummings Thatia alijitengenezea tembe zilizojulikana kama Viagra Pro na kisha kuuzia wateja wake.

Mamlaka ya Ushuru (KRA) mwaka jana iliharibu shehena ya tembe zilizodaiwa kuongeza hamu ya mapenzi zilizonaswa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Eldoret.

Kulingana na KRA shehena hiyo ilikuwa ikielekea mjini Nakuru lakini mwenyewe alikosa kujitokeza baada ya mzigo wake kunaswa.Soko la tembe za kuongeza hamu ya mapenzi linakua kwa kasi humu nchini.

“Wengi hawajui kuwa kununua tembe za Viagra dukani ni kinyume cha sheria na wanaweza kukamatwa. Tembe hizo zimeidhinishwa kwa ajili ya matibabu yanayotolewa na daktari na wala si kuzitumia kiholela katika starehe,” anasema Dkt Ikamati.

Dkt Ikamati anasema kuwa kutazama video za ngono ni miongoni mwa sababu zinazochochea watu, haswa vijana, kukimbilia tembe za kuongeza hamu ya mapenzi au nguvu za kiume.

Anasema kuwa wanaume wanaotazama video hizo chafu kwa muda mrefu hukosa nguvu za kiume au hudumu kwa muda mfupi wakati wa kufanya mapenzi.

Dkt Ikamati, hata hivyo, anasema kuwa tembe halali za Viagra zikitumiwa kwa kuzingatia maelekezo ya daktari zinaweza kusaidia watu walio na matatizo ya nguvu za kiume.

“Lakini tembe hizo zikitumiwa kiholela zinaweza kudhuru afya na hata kusababisha kifo. Ikiwa mwathiriwa anatumia aina fulani za dawa za presha, maradhi ya moyo au kisukari anaweza kufariki ghafla iwapo atameza Viagra. Hii ni kwa sababu dawa hizo huwa na ‘nitrate’ ambayo ikikutana na Viagra husababisha presha ya damu kushuka ghafla kuliko kawaida na kusababisha kifo,” anaelezea.

Mtu aliye na maradhi ya selimundu (sickle cell), vidonda vya tumbo, upungufu wa damu (anemia) matatizo ya ini, nakadhalika, hawafai kutumia Viagra.Matumizi ya Viagra kiholela kwa muda mrefu, Dkt Ikamati anaonya, yanamfanya mwanaume kuwa goigoi kitandani katika siku za usoni kwani tembe zitakosa uwezo wa kusisimua mwili.

Mnamo 2017, bodi ya PPB ilielezea wasiwasi wake kuhusu ongezeko la watu wanaotumia tembe za kuongeza hamu ya ngono katika maeneo ya Pwani.Bodi hiyo iliwataka wakazi wa Pwani kuripoti wauzaji wa tembe za kuongeza hamu ya mapenzi kwa watu wasiokuwa na barua ya daktari.

You can share this post!

Viongozi wa Magharibi waitetea IEBC

Kiini cha kufifia kwa nguvu za kufanya mapenzi